Habari Mseto

Aliyetaka kulipwa Sh300,000 na kundi la WhatsApp kwa kufiwa azimwa mahakamani

Na BRIAN OCHARO March 3rd, 2026 Kusoma ni dakika: 3

MAHAKAMA ya Madai Madogo jijini Mombasa imetupa nje kesi ya mwanachama wa kundi la WhatsApp aliyetaka kundi hilo lilazimishwe kumlipa Sh300,000 kufuatia msiba wa kifamilia.

Bw Nicholas Ogola alishtaki kikundi cha Luo Professionals (LUP) Welfare Group, akiwatuhumu maafisa wake kwa kushindwa kuhamasisha wanachama kumsaidia wakati wa msiba wake.

Alisema kuwa kundi hilo, lililoanzishwa kama jukwaa la ustawi wa kitaaluma, lilitarajiwa kutoa msaada wa kifedha kwa wanachama wakati wa mahitaji kama vile mazishi.

Bw Ogola alikuwa ameomba mahakama iamuru achangiwe fedha za kugharimia mazishi kufuatia kifo cha mamake wa kambo.

Mahakama ilitegemea masharti ya msiba yaliyo katika katiba ya kundi hilo, ambayo yanaruhusu msaada wa kifedha kwa mwanachama iwapo atampoteza mzazi mlezi.

“Hata hivyo, mzazi mlezi au mlezi huyo lazima awe ametangazwa na mwanachama huyo kwa kundi la ustawi. Mlalamishi katika kesi hii, kama alivyokiri, hakuwa amemtangaza ipasavyo Caren Akello Ogola kama mama wa kambo, mzazi mlezi au mlezi wake,” mahakama ilisema.

“Kwa kuzingatia hayo, na kwa mtazamo wa yaliyoelezwa hapo juu, hitimisho lisiloepukika ambalo mahakama lazima ifikie ni kwamba kesi ya mlalamishi haikuthibitishwa kwa kiwango kinachotakiwa. Kwa hivyo, inatupiliwa mbali,” mahakama ikaeleza.

Kwa kuzingatia idadi ya wanachama na michango iliyotarajiwa kutoka kwa kila mmoja, Bw Ogola alisema alitarajia kupokea karibu Sh300,000 ili kumpa mama yake wa kambo “mazishi ya heshima.”

Aliwalaumu maafisa wa kundi hilo, akiwemo mwenyekiti Pius Oketch na mweka hazina Morris Abwao, kwa kushindwa kuhamasisha wanachama kutoa michango yao binafsi alipompoteza mamake wa kambo.

Mbali na Sh300,000 alizodai, alitaka pia kinga dhidi ya kufukuzwa uanachama kwa kudai haki yake.

Kulingana naye, marehemu Caren Akello Ogola alikuwa mama yake wa kambo na mlezi aliyemlea baada ya kifo cha awali cha mama yake mzazi.

Alisema amekuwa akichangia kwa uaminifu katika misiba ya wanachama wengine na hivyo alishtushwa mwenyekiti alipokataa ombi lake la msaada.

“Ingawa marehemu hakuwa mama yangu mzazi, ndiye aliyenilea,” alisisitiza.

Kuthibitisha madai yake, aliwasilisha katiba ya kundi, kijitabu cha rambirambi kilichomworodhesha miongoni mwa watoto wa marehemu, nakala ya kitambulisho cha taifa cha marehemu na cheti chake cha kuzaliwa.

Hata hivyo, cheti cha kuzaliwa kilionyesha kuwa mama yake mzazi alikuwa Cecilia Anne Jole.

Kwa upande wa utetezi, mwekahazina wa kundi hilo, Bw Abwao, aliyetoa ushahidi kwa niaba ya washtakiwa wote, alikiri kuwa Bw Ogola ni mwanachama halali.

Alisisitiza kuwa, kulingana na taarifa za kibinafsi ambazo Bw Ogola aliwasilisha, mama huyo wa kambo hakukidhi vigezo vya LUP Welfare Group vya kutoa msaada wakati mwanachama anapofiwa.

“Suala la mama wa kambo wa mlalamishi kumlea halikuwepo katika arafa zake. Kwa hakika, arafa zilionyesha kuwa mjomba ndiye aliyemlipia masomo,” alisema Bw Abwao.

Kulingana naye, msaada wa kifedha hutokana na michango ya kila tukio, si kutoka kwa hazina ya kudumu, kwani kundi halikuwahi kuwa na fedha taslimu zilizokuwa zikingoja kutolewa kwa msiba.

Kulingana na rekodi zilizowasilishwa mahakamani, Bw Ogola alikuwa amemtaja Carolina Ogola kama mama yake na akaonyesha kuwa baba yake alikuwa amefariki.

Hivyo basi, alipowafahamisha viongozi kuhusu kifo cha mama yake wa kambo, maafisa waliamua kutoanzisha zoezi la michango.

Bw Abwao aliiambia mahakama kuwa ingawa Bw Ogola alikuwa huru kuomba msaada kutoka kwa marafiki, wakiwemo wanachama wa kundi kwa hiari yao binafsi, mama wa kambo hakuwa ametangazwa kama mnufaika katika rekodi rasmi.

Aliongeza kuwa hata pale ambapo mnufaika aliyetangazwa anafariki, michango ni ya hiari na si haki ya moja kwa moja kwa wanachama.

“Wakati wowote, si wanachama wote huchangia,” alisema, akihoji jinsi kiwango cha Sh300,000 alichodai Bw Ogola kingehakikishwa.

Washtakiwa pia waliiambia mahakama kuwa uamuzi wa kutohamasisha msaada ulipowasilishwa kwa Bw Ogola na Katibu Mkuu, alijibu kwa kumtukana.

Kwa kutupilia mbali dai la Sh300,000, mahakama ilihitimisha kuwa marehemu hakuwa ametangazwa katika taarifa za kibinafsi za kundi la ustawi, hivyo kundi hilo halingeweza kulazimishwa kulipa fedha hizo.

Kuhusu ombi la Bw Ogola la kutofukuzwa uanachama, mahakama ilikataa kuingilia kati, ikibainisha kuwa, kundi hilo lina katiba madhubuti inayoweza kushughulikia masuala ya ndani, na ikaamua kuwa halikuwa na mamlaka ya kuingilia eneo hilo.