Habari Mseto

Bei ya nyama yapanda maradufu wateja nao wakipotea na kuacha wenye bucha matatani

Na MICHAEL OCHIENG', JACKSON NGARI April 3rd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

BEI ya nyama ya ng’ombe nchini imepanda kwa kiasi kikubwa katika miezi ya hivi karibuni, huku kilo moja ikiuzwa sasa kati ya Sh750 na Sh900 katika masoko na maduka ya nyama, kutoka karibu Sh400 mnamo 2020.

Ongezeko hili limeathiri wateja na wauzaji kwa kiasi kikubwa mashinani, ambapo baadhi ya wamiliki wa maduka na wauzaji wanasema idadi ya wateja imepungua, jambo linalowalazimu kuangalia upya njia za kuendesha biashara zao.

Kulingana na Mkuu wa Mauzo katika Kampuni ya Nyama nchini (KMC), Lydia Mandila, ongezeko la bei za nyama linahusiana hasa na mabadiliko ya hali ya hewa na bei ya mifugo.

Alifafanua kuwa msimu wa mvua unasababisha wakulima kuhifadhi mifugo yao ili kuinenepesha badala ya kuuza sokoni.

“Mvua inaponyesha, wakulima huhodhi mifugo ili kuinenepesha. Hii hupunguza bidhaa sokoni. Wakati huo huo, wateja huzidi kuongezeka, na kusukuma bei juu,” alisema Bi Mandila.

Aliongeza kwamba ingawa KMC huchangia katika ununuzi, na usambazaji wa nyama, ina udhibiti mdogo kuhusu bei kwani viwanda vya nyama vingi vinajitegemea sokoni.

Aidha, wengi wa Wakenya hununua nyama kutoka kwa vituo vidogo vya kuchinja ambavyo haviko rasmi, jambo linalofanya kudhibiti bei kuwa kugumu.

Kiini cha ongezeko la bei ni pia kupanda kwa bei za mifugo.

“Mwaka huu, bei za mifugo zimepanda maradufu. Kawaida hupanda Desemba na kushuka kati ya Januari na Machi, lakini mwaka huu mvua imekuja mapema, na bei ziko juu zaidi ya Desemba. Kwa jumla, bei zimepanda karibu asilimia 40 ikilinganishwa na mwaka jana,” alifafanua.

Licha ya bei za juu, KMC inasema idadi ya wateja haijapungua, badala yake imeongezeka.

“Sio kupata faida kubwa tunalenga. Kiwango chetu ni cha chini mno, hivyo wateja wanatujia kwa sababu bei zetu ni nafuu,” alisema Bi Mandila.

Ongezeko la bei za nyama limeonyesha jinsi soko la nyama nchini linavyotegemea hali ya hewa, bei za mifugo na tabia za walaji, huku wauzaji wakikabiliana na changamoto za kudhibiti bei katika viwanda na masoko yasiyo rasmi.