Habari Mseto

Bodaboda waua ‘afisa wa polisi’ aliyeshukiwa kujihusisha na ujambazi

Na DOMNIC OMBOK, KAMORE MAINA February 19th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

VISA viwili vya wizi wa kutumia nguvu vilivyotokea katika kaunti tatu vimeibua tena hofu kuhusu mtindo unaochipuka wa maafisa polisi wasio waadilifu kuvuka mipaka ya kaunti kutekeleza uhalifu dhidi ya raia waliokula kiapo kuwalinda.

Jumanne asubuhi, wakazi wa Kisumu na Kericho waliwaua washukiwa watano wa ujambazi, mmoja wao akapatikana na kitambulisho cha polisi.

Washukiwa hao walijitambulisha kwa Mweka Hazina wa Mashambani Farmers’ Cooperative Society Richard Bala, kama maafisa wa polisi muda mfupi baada ya kutoka tawi la Kenya Commercial Bank (KCB) Muhoroni akiwa na Sh1.1 milioni.

Hata hivyo, polisi wamedai kitambulisho kilichopatikana eneo la tukio ni bandia na kina maelezo ya maafisa wawili tofauti.

Msemaji wa Huduma ya Polisi, Muchiri Nyaga, jana alisema nambari ya huduma iliyo kwenye kitambulisho hicho ni ya afisa mwingine aliye kazini Kasarani.

Afisa mkuu wa Kituo cha Polisi cha Koru alisema hawana afisa kwa jina lililo kwenye kitambulisho hicho, huku afisa mwingine akidai jina hilo ni la konstebo aliye Busia.

Bw Nyaga alisema wachunguzi bado hawajawatambua washukiwa.

“Tumekusanya alama za vidole na tunatarajia matokeo hivi karibuni,” alisema.

Washukiwa hao walimlazimisha Bala kuingia kwenye gari lao na kuelekea Kericho. Wananchi, wakiwemo waendesha bodaboda, waliwafuatilia na kuwazingira wakiwa Koitaburot, Kaunti ya Kericho.

Polisi walipofika walifyatua risasi, moja ikimpata Irine Chepkemoi ambaye bado anapatiwa matibabu hospitalini.

Haijabainika iwapo alikuwa sehemu ya umati.

Tukio hilo lilitokea takriban saa 24 kabla ya afisa wa polisi wa Kisumu, Mark Owino, kusimama katika gwaride la utambuzi kutambuliwa iwapo ni miongoni mwa watu watatu waliomvamia mfanyabiashara na wateja watatu Ajigo, Kaunti ya Siaya, Februari 2.