• Nairobi
  • Last Updated May 1st, 2024 10:08 PM
Chifu na mwanawe taabani kwa tuhuma za mauaji ya mfanyakazi

Chifu na mwanawe taabani kwa tuhuma za mauaji ya mfanyakazi

NA KITAVI MUTUA

MAKACHERO katika Kaunti ya Kitui wanachunguza kisa cha Chifu wa lokesheni ya Kavuta eneo la Kitui ya Kati na mwanawe kushukiwa kuhusika katika mauaji ya aliyekuwa mfanyakazi wake wa shambani.

Bw Billy Muthui Musembi alikamatwa wikendi na kuzuiliwa katika Kituo cha Polisi cha Itoleka, Kaunti Ndogo ya Katulani, baada ya miezi kadhaa kukwepa mtego wa kunaswa na wapelelezi.

Bw Musembi na mwanawe, Bw Thomas Jefferson Muthui wanadaiwa kumpiga hadi kumuua aliyekuwa mfanyakazi wao wa shambani, Marehemu Peter Musee Musomba mchana peupe mnamo Desemba 19, 2024, ndani ya boma lao.

Baada ya tukio hilo, msimamizi huyo aliomba likizo ya siku 45 lakini alijificha na kuzima simu yake ya mkononi, hadi mwezi uliopita aliporejea kazini.

Kulingana na maafisa wa upelelezi wanaochunguza kisa cha mauaji, mfanyakazi huyo wa shambani alikuwa ameenda kudai malipo yake ya kazi aliyofanya wakati chifu huyo na wanafamilia wengine walipomshtumu kwa kuiba mahindi kutoka kwa duka lao.

Siku hiyo, Chifu aliratibiwa kumkaribisha Mbunge wa Kitui ya Kati, Bw Makali Mulu katika mkutano wa umma katika soko la Kavuta, Wadi ya Changwithya Magharibi ambapo basari zilitolewa kwa wanafunzi walio na mahitaji katika eneo hilo.

“Mabadiliko hayo na aliyekuwa shamba boi yalitokea kabla ya baraza la umma la mbunge kuanza na kushuhudiwa na majirani kadhaa na wapita njia,” mdokezi wetu akasema.

Kisha walimfunga mikono na kumuadhibu kwa kutumia fimbo na vifaa vingine butu hadi akapoteza fahamu.

Madai ya wizi hayakuwahi kuripotiwa kwa polisi.

Kabla ya kuondoka kwenda kazini, msimamizi huyo alimwagiza mtoto wake kumbeba mhanga huyo ambaye bado alikuwa hai kumtoa nje ya nyumba yao, ambapo alimtupa mfanyakazi huyo kando ya barabara inayounganisha Mangina na Kwa Mukasa, umbali mfupi kutoka nyumbani kwa Chifu.

Mfanyakazi huyo hakuwahi kuamka kutoka mahali alipotupwa kwani alikufa kutokana majeraha mchana huo huo.

Katika mkutano wa umma, Chifu alizima simu yake ya mkononi, baada ya kuhisi huenda mfanyakazi wa shambani amefariki.

“Watu wa kwanza kufika eneo la tukio walijaribu kumtafuta chifu huyo kwa simu yake ya mkononi ili kumjulisha kuhusu kupatikana kwa maiti katika eneo lake lakini simu yake ilikuwa imezimwa, wakamtuma mhudumu wa bodaboda kwenda kumfikishia ujumbe huo katika mkutano,” alisimulia afisa wa polisi ambaye hakutaka kurekodiwa kwa sababu haruhusiwi kuzungumza na wanahabari.

Mkurugenzi wa Upelelezi wa Jinai (DCI) Kaunti ya Kitui, Mhandisi Samwel Bett alithibitisha kukamatwa kwa Chifu huyo akisema atafikishwa mahakamani kujibu mashtaka ya mauaji.

Data ya simu ya rununu kutoka Safaricom ambayo iliwaweka washukiwa wote katika eneo la uhalifu ni miongoni mwa ushahidi utakaotumika kortini.

 

  • Tags

You can share this post!

Wizara ya Kilimo kutuma wakaguzi kutekeleza kanuni za miraa

CIPK yaomba serikali kutopuuzilia mbali mkataba na madaktari

T L