• Nairobi
  • Last Updated April 30th, 2024 10:55 AM
Junet hatarini kunyakwa na EACC kwa ufisadi

Junet hatarini kunyakwa na EACC kwa ufisadi

BRIAN WASUNA na RICHARD MUNGUTI

MBUNGE wa Suna Mashariki, Bw Junet Mohammed, yumo hatarini kunyakwa na makachero wa Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC) kwa kuhusishwa na sakata ya ufisadi wa Shirika la Huduma za Vijana kwa Taifa (NYS).

Imefichuka kuwa, Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP), Bw Noordin Haji tayari ameidhinisha kesi ziendelezwe dhidi ya washukiwa wapya wa sakata ya kwanza ya NYS.

Uchunguzi wa EACC umeonyesha kuwa, mbunge huyo ambaye ni mwandani wa karibu wa Kiongozi wa ODM, Raila Odinga, anashukiwa alinufaika kwa fedha zilizofujwa.

Sakata hiyo iliyohusisha ufujaji wa Sh1.9 bilioni ulitikisa utawala wa Rais Uhuru Kenyatta katika awamu yake ya kwanza ya uongozi.

Katika mwaka wa 2015, Bw Mohamed alihusishwa na kampuni mbili zilizosambaza bidhaa za Sh129 milioni kupitia kwa zabuni za NYS ambazo zilitiliwa shaka.

Hata hivyo, wapelelezi wameamua kutilia maanani zabuni ambayo ilipeanwa kwa kampuni ya Zeigham Enterprises, ambapo Bw Mohamed ni mmoja wa wakurugenzi.

Zeigham Enterprises ilipewa kandarasi ya kuuzia NYS vifaa mbalimbali vilivyogharimu Sh21.8 milioni.

Uchunguzi umesema, baada ya Zeigham kupokea fedha hizo, kiasi fulani kilitumwa kwa akaunti ya benki ya Waziri Msaidizi wa Michezo Hassan Noor Hassan, na mkewe, Bi Meymuna Sheikh Nuh ambaye ni dadake Bw Mohamed.

Wakati huo, Bw Hassan alikuwa akifanya kazi katika Wizara ya Ugatuzi iliyokuwa ikisimamiwa na Bi Anne Waiguru, na ndiye alikuwa mwenyekiti wa kamati ya zabuni iliyochagua kampuni ya Zeigham.

Makachero wa EACC wamethibitisha kulikuwa na doa katika utoaji wa zabuni hiyo, kwani watu wengine wanaohusishwa na kampuni hiyo ni jamaa za Bw Mohamed.

Kakake mbunge huyo, Bw Hussein Mohamed Haji, pia ni mkurugenzi wa Zeigham Enterprises.

You can share this post!

ONGAJI: Ukosefu wa kazi umeumbua na kudhalilisha vijana wetu

Monaco wampokeza mikoba kocha Niko Kovac

adminleo