Habari Mseto

Kazini ndio kwenye unyanyasaji mkubwa zaidi wa kimapenzi Afrika – Utafiti wa GeoPoll

Na KAMAU MAICHUHIE March 30th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MAHALI pa kazi ndilo eneo hatari zaidi kwa unyanyasaji wa kingono barani Afrika, huku zaidi ya nusu ya wafanyakazi katika nchi nne wakisema wamekumbana na hali hiyo, na wanawake wakibeba mzigo mkubwa zaidi.

Haya ni kwa mujibu wa ripoti mpya ya usawa wa kijinsia iliyotolewa na GeoPoll, iliyochunguza hali hiyo nchini Kenya, Nigeria, Afrika Kusini na Misri.

Ripoti hiyo ilibaini kuwa asilimia 51 ya washiriki wamewahi kukumbana na unyanyasaji wa kingono kazini, huku pengo kati ya wanaume na wanawake likiwa kubwa kwa asilimia 25.

Takriban wanawake sita kati ya kumi, sawa na asilimia 59, walisema wamepitia unyanyasaji huo binafsi, ikilinganishwa na asilimia 35 ya wanaume.

Kwa ujumla, karibu nusu ya waliohojiwa, asilimia 47, walikiri kuwa wamewahi kukumbana na aina fulani ya unyanyasaji wa kingono, kuanzia maneno na ishara zisizofaa hadi kuguswa kimwili.

Ripoti hiyo inaeleza kuwa wanawake si tu hulengwa zaidi, bali pia hukumbwa na unyanyasaji kwa kiwango kikubwa. Hata hivyo, inasisitiza kuwa tatizo hilo si la wanawake pekee, kwani mwanaume mmoja kati ya watatu pia ameripoti kukumbana na hali hiyo.

Changamoto kubwa inayozuia kukabili tatizo hili ni kutoripotiwa kwa visa vingi. Utafiti unaonyesha kuwa ingawa mwanamke mmoja kati ya wawili hupitia unyanyasaji kazini, ni asilimia 30 tu ya visa vinavyoripotiwa.

Wengi huogopa kulipiziwa kisasi au hukosa imani kuwa hatua zitachukuliwa.

Uhalisia wa changamoto hii ulionekana katika kesi moja jijini Nairobi mwaka jana, ambapo Mahakama ya Ajira na Leba iliamua kuwa kufutwa kazi kwa wakili mmoja katika shirika la Kituo cha Sheria hakukuwa halali, na kuamuru alipwe fidia ya Sh1.5 milioni.

Wakili huyo alifutwa kazi baada ya mfanyakazi wa kiume kumshutumu kwa unyanyasaji wa kingono, akidai alimtaja kwa majina kama “baby boy” na “boy lollipop” bila idhini yake.

Mahakama pia ilipata kuwa mwajiri hakumpa mhusika nafasi ya kujitetea ipasavyo.