Habari Mseto

Kitendawili cha mbolea kukosekana msimu wa upanzi ukianza

Na BARNABAS BII March 22nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SERIKALI inakabiliwa na kitendawili kigumu kusawazisha kati ya kuongeza uzalishaji wa mimea na kuwepo chakula cha kutosha kutokana na upungufu wa mbolea ya bei nafuu.

Hii ni licha ya mipango ya kununua kutoka nchi za kigeni mifuko 12.5 milioni ya kilogramu 50 yenye thamani ya Sh15 bilioni msimu huu.

Mbolea ya bei nafuu inayouzwa kwa Sh2,500 kwa sasa haipatikani katika mabohari mengi ya Bodi ya Kitaifa ya Nafaka na Mazao (NCPB) katika maeneo yote muhimu kwa ukuzaji wa mahindi.

Haya yanajiri wakulima wakianza msimu wa upanzi, huku Wizara ya Kilimo ikihusisha upungufu uliopo na changamoto za usafirishaji na idadi inayozidi kuongezeka ya wakulima wanaohitaji bidhaa hiyo.

Wakulima wa mahindi katika eneo la Bonde la Ufa Kaskazini walivamia mabohari ya NCPB kulalamikia upungufu huo, wakisema unatatiza ratiba zao za upanzi.

Taifa linahitaji karibu tani 650,000 za mbolea kila mwaka, lakini baadhi ya wakulima huenda wakalazimika kupanda bila kuweka virutubishi hivyo kutokana na bei ghali ya mbolea inayouzwa dukani.

Msimu wa upanzi katika Bonde la Ufa Kaskazini, eneo linalokuza chakula kwa wingi nchini, kwa kawaida huanza kati ya Februari na Machi.

Hata hivyo, mabadiliko ya mara kwa mara ya hali ya anga huenda yakachelewesha shughuli hiyo hadi Aprili, hali ambayo wataalam wa kilimo wameonya kuwa huenda ikasababisha mazao duni.

Serikali kufikia sasa imesambaza mifuko 3.2 milioni ya kilogramu 50 za mbolea tangu Disemba 2025 kupitia mabohari ya NCPB na vituo vya usambazaji mashinani.

Serikali ya Kenya Kwanza ilitengea mbolea ya bei nafuu Sh12 bilioni katika msimu uliopita wa upanzi, lakini mchakato wa usambazaji umeandamwa na kashfa tele zilizosababisha aliyekuwa waziri wa kilimo Mithika Linturi kufutwa kazi katika mabadiliko ya Baraza la Mawaziri.

Kulingana na Rais William Ruto, nchi hutumia takriban Sh500 bilioni kila mwaka kwa bidhaa za chakula zinazonunuliwa kutoka mataifa ya kigeni.

Serikali yake inalenga kupunguza kiasi hiki kupitia vifaa vya kilimo kwa bei nafuu na kutumia mashine kuimarisha uzalishaji nchini.

Hata hivyo, juhudi za kulainisha usambazaji wa mbolea kupitia vituo vya NCPB msimu uliopita ziliathiriwa na kashfa.

Mbolea ya bei nafuu kwa sasa inasambazwa kupitia vituo vya NCPB, vyama vya ushirika wa wakulima, vituo mashinani na wauzaji wa vifaa vya kilmo wenye leseni.