Habari Mseto

Korti yaruhusu madalali kuvamia makazi ya mbunge kufuata deni la Sh7.5 milioni

Na JOSEPH OPENDA June 11th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

MAHAKAMA Kuu ya Nakuru imeruhusu madalali kuvamia kwa nguvu nyumba ya Mbunge wa Naivasha, Bi Jayne Kihara, ili kukusanya deni la Sh7.5 milioni anazodaiwa na aliyekuwa mbunge, John Mututho.

Jaji Julius Nangea alitoa agizo kuwapa madalali walioteuliwa na Bw Mututho ruhusa ya kuingia na kutwaa mali ya mbunge huyo kuuza mnadani.

Kamanda wa Kituo cha Polisi cha Naivasha ameagizwa kusimamia operesheni hiyo na kuhakikisha agizo la mahakama linatekelezwa ipasavyo.

“Agizo la kuvunja lango limetolewa kwa niaba ya mlalamishi wa tatu (Mututho), likimruhusu, kupitia kwa madalali wake alioteua wa kampuni ya Impair Group of Companies, kuvunja na kuingia kwenye makazi ya mshtakiwa (Kihara) huko Maraigushu, Eneo Bunge la Naivasha, kutekeleza agizo la mahakama kuhusu deni linalodaiwa,” aliamua Jaji Nangea.

Kiasi hicho ni sehemu ya gharama za kesi iliyotolewa na mahakama kufuatia kesi ya kupinga matokeo ya uchaguzi iliyowasilishwa dhidi yake na Bi Kihara mwaka wa 2008.

Mahakama ilitoa uamuzi kukubaliana na Bw Mututho mnamo Desemba 19, 2019, ikimfidia Sh7.5 milioni pamoja na riba.Licha ya uamuzi huo, Bw Mututho alirejea mahakamani akidai kuwa Bi Kihara alikuwa akizuia juhudi za kukusanya deni hilo.

Alidai kuwa madalali wake walifukuzwa kwa nguvu kutoka nyumbani kwa mbunge huyo walipojaribu kutekeleza agizo la mahakama.

Bw Mututho, ambaye aliwahi kuwa mwenyekiti wa Mamlaka ya Kitaifa ya Kupambana na Matumizi ya Dawa za Kulevya (Nacada), alimshutumu zaidi mbunge huyo kwa kutumia kesi mahakamani kuchelewesha na kuzuia utekelezaji wa hukumu hiyo.

Kesi zote zilizowasilishwa na Bi Kihara zilitupiliwa mbali. Mahakama iliambiwa kuwa Bi Kihara aliwaandikia madalali akipendekeza mkutano wa kupanga malipo, lakini mkutano huo haukufanyika.

Mnamo Oktoba 18, 2023, madalali walijaribu kutekeleza agizo lililotolewa Septemba 29, 2023, lakini walikumbana na upinzani mkali kutoka kwa walinzi.

Hapo awali, mahakama ilimfidia Sh7.5 milioni ambazo sasa zimeongezeka hadi Sh10,988,786 milioni kutokana na riba. Inaripotiwa kuwa Mbunge Kihara alilipa Sh3 milioni kabla ya juhudi za kukusanya kiasi kilichobaki kusitishwa.

Katika uamuzi wake, Jaji Nangea alibaini kuwa hakuna agizo lolote lililotolewa kusitisha utekelezaji wa hukumu hiyo, isipokuwa rufaa zilizowasilishwa.

Alimlaumu mbunge huyo kwa kuvuruga utekelezaji wa kisheria wa hukumu hiyo bila sababu ya msingi.