Habari Mseto

Korti yatupa rufaa ya mwanamke aliyenajisi mvulana

Na PHILIP MUYANGA September 27th, 2024 1 min read

MWANAMKE aliyenajisi mvulana mwenye umri wa miaka 14 katika Kaunti ya Tana River, ataendelea kuhudumu kifungo cha miaka 20 baada ya mahakama kutupilia mbali rufaa yake dhidi ya hukumu hiyo.

Mahakama ya Rufaa ilisema ushahidi wa upande wa mashtaka dhidi ya Magaret Nyokabi ulikuwa mzito, kwamba alimnajisi mvulana huyo ambaye wakati huo alikuwa darasa la sita mara kadha na hakuonyesha majuto baada ya kuhukumiwa.

Majaji wa Mahakama ya Rufaa Gatembu Kairu, Lydia Achode na George Odunga walisema kifungo alichopewa Bi Nyokabi kilikuwa ni mwafaka kulingana na makosa aliyoyafanya.

Bi Nyokabi alikuwa amehukumiwa na mahakama ya hakimu mjini Hola baada ya kupatikana na hatia ya kumnajisi mvulana huyo.

Alikata rufaa ya uamuzi huo katika Mahakama Kuu ambayo ilitupa rufaa hiyo na bado akakata rufaa ya pili katika Mahakama ya Rufaa.

Mahakama ya Rufaa ilisema kuwa Bi Nyokabi hakuwa ameonyesha ni kwa njia ipi alikuwa amebaguliwa au vile haki yake ilikuwa imekiukwa wakati wa kusikizwa kwa kesi yake.