Habari Mseto

Mabilioni yatengwa kunyanyua uchumi

May 24th, 2020 1 min read

NA MWANDISHI WETU

RAIS Uhuru Kenyatta ametangaza juhudi atakazoweka ili kufufua uchumi wa nchi. Mikakati hiyo itahusisha mabilioni ya fedha kunyanyua hali ya biashara nchini na kuendeleza miradi ya serikali.

Sh5 bilioni zitatumika kuajiri wafanyikazi wadogo wadogo wa kukarabati barabara na njia wakati wa mafuriko.

Sh6.5 bilioni zimetengewa Wizara ya Elimu ili kuajiri walimu 10,000, kuajiri wakufunzi wa mitandaoni 10,000 na kununua madawati ya wanafunzi.

Sh10 bilioni zitatumika katika uchunguzi wa ulipaji wa ushuru na Sh3 bilioni kwa wafanyabiashara wadogo wadogo.

“Tutatafuta njia ya kufungua biashara tena huku tukijizoesha kuishi na virusi vya corona”, Rais alisema  Jumamosi.

Sh1.7 bilioni zitatumika kuongeza vitanda hospitalini na kuajiri madaktari 5,000. Sh3 bilioni zimetengwa kwa kusafirishwa mazao ya shambani huku Sh1.5 milioni zikitumika kusaidia wakulima wa maua na masoko ya kimataifa.

Sh2 bilioni zitatumika kusaidia sekta ya hoteli kwa kuwapa wamiliki mikopo huku Sh1 bilioni zikitengewa kukabiliana na mafuriko na Sh850 milioni kutengeneza visima na matangi ya maji.

Sh540 milini zimetengwa kusaidia katika kampeni ya kuhifadhi mazingira, Sh600 milioni kupiga jeki sekta ya viwanda.

“Ninawahimiza Wakenya tuwe wazalendo daima tukiwa na imani kuwa tutashinda,” akasema.

Alisema kuwa bado familia zenye mapato ya chini zinazoathirika zaidi zitaendelea kupata pesa kila wiki.

Tafsiri: Faustine Ngila