• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 6:55 AM
Maporomoko yaua 4 mvua ikizidi kutatiza

Maporomoko yaua 4 mvua ikizidi kutatiza

Na EVANS KIPKURA na KALUME KAZUNGU

WATU wanne wa familia moja walikufa pale nyumba yao iliangukiwa na maporomoko ya ardhi yaliyosababishwa na mvua kubwa katika kijiji cha Turung, Kaunti ya Elgeyo-Marakwet.

Polisi walisema kuwa kisa hicho kilitokea Alhamisi usiku watu hao walipokuwa wakilala.

Mkuu wa polisi eneo la Marakwet Mashariki (OCPD) Vincent Kitili alisema miili ya mwanamume, mkewe na watoto wao wawili ilipatikana Ijumaa asubuhi.

Mnamo Jumatano, watu wanne walikufa gari lao liliposombwa na mafuriko katika Kaunti ya Kitui.

Katika Kaunti ya Lamu mamia ya wakazi kwenye vijiji vilivyoko msitu wa Boni, wameathiriwa na mafuriko baada ya mto Lagwarera ambao unaanzia Ethiopia kuvunja kingo zake.

Mapema Oktoba, mto Lagwarera ulivunja kingo na kuathiri baadhi ya miji ya Kaskazini mwa Kenya, ikiwemo Marsabit na Mandera.

Juma hili, wakazi wa vijiji vya Bodhei, Milimani, Mararani, Mangai na Bar’goni, Kaunti ya Lamu walianza kuhisi athari za mto Lagwarera baada ya mafuriko kuharibu madaraja matatu kwenye barabara kuu ya Hindi kuelekea Kiunga.

Shughuli za usafiri eneo hilo kwa sasa zimekatizwa kabisa kufuatia mafuriko hayo ambayo pia yamepelekea barabara kukatika sehemu tofauti.

Wakulima kwenye vijiji vya Mangai, Mararani na Milimani pia wameripotiwa kukadiria hasara baada ya mimea yao kusombwa na maji ya mafuriko.

Wanafunzi waathirika

Wanafunzi wa shule pia ni miongoni mwa walioathirika zaidi na mafuriko hayo kwani takriban wanafunzi 170 kutoka kijiji cha Bodhei ambao husomea shule ya msingi ya Ijara hawajafika shuleni kwa siku tatu.

Kufikia Alhamisi, madereva wa malori ya kusafirisha vyakula na bidhaa nyingine kutoka Lamu Magharibi hadi vijiji vya Lamu Mashariki walikuwa wamesitisha shughuli zao wakisubiri maji kupungua.

Katika mahojiano na wanahabari Ijumaa, Mwakilishi wa Wadi ya Basuba, Bw Barissa Deko alieleza wasiwasi wake kwamba huenda wakazi wa vijiji husika wakaumia kwa njaa iwapo hatua za dharura hazitachukuliwa kuwapelekea msaada wa chakula.

Bw Deko pia aliitaka serikali na wahisani kujitokeza na kusambazia wakazi vyandarua vya kuwakinga dhidi ya mbu na dawa za kutibu maji machafu ili kuzuia mkurupuko wa maradhi yanayosababishwa na mafuriko.

“Hapa Boni mvua hainyeshi lakini cha kustaajabisha ni kwamba mto wa Ethiopia uliovunja kingo zake hivi majuzi umetuathiri. Mito yetu, ikiwemo ule wa Mangai, Milimani na Mararani tayari imevunja kingo baada ya kupokea maji kutoka Ethiopia. Hali hiyo imesababisha mafuriko na kutatiza shughuli za usafiri. Wakazi sasa hawawezi kutembea kutoka kijiji kimoja hadi kingine kujinunulia chakula. Serikali ifikirie kuwapelekea wakazi wa hapa chakula cha msaada hata kama ni kwa kutumia usafiri wa ndege,” akasema Bw Deko.

Bw Ali Guyo ambaye ni mkulima wa Mararani alisema mimea mingi mashambani mwao imefagiliwa na maji ya mafuriko.

Bw Guyo aliiomba serikali kufikiria kuwafidia wakulima wote wa msitu wa Boni ambao wameathiriwa na mafuriko hayo la sivyo watakabiliwa na baa la njaa.

  • Tags

You can share this post!

BBI ndiyo dawa ya maridhiano, asema Waiguru

Buhari aanza kufunga shule za Kiislamu zilizogeuka...

adminleo