• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 12:09 PM
Mzee aliyehonga jaji azirai ghafla mahakamani

Mzee aliyehonga jaji azirai ghafla mahakamani

Na RICHARD MUNGUTI

MAMBO yalimwendea mrama MZEE mwenye umri wa miaka 67  anayeshtakiwa kujaribu kumhonga Jaji Roselyn Aburilili  wa Mahakama kuu Milimani Nairobi.

Kwa ghafla Mzee Joseph Wainaina alianza kutokwa na jasho na kuishiwa na nguvu.

Alijaribu kusimama lakini akashindwa hata ikabidi hakimu mwandamizi Lawrence Mugambi kumtaka mshtakiwa akae kwanza apate afueni.

Dau la Mzee Wainaina lilipigwa na mawimbi ya hofu na woga aliposikia jina lake limetajwa karani wa Jaji Aburili , Bi Adeline Shitawa Murunga aliposomewa mashtaka.

Mzee huyo alikabiliwa na shtaka la kumpa mlungula Bi Murunga ndipo amshawishi Jaji Aburili ampendelee akitoa uamuzi katika kesi aliyokuwa ameshtaki.

Mzee  Wainaina kutoka kaunti ya Murang’a alishtakiwa kwa kumpa Bi Murunga, aliyekuwa karani wa Jaji Aburili Sh50,000 ndipo atweze haki katika kesi aliyokuwa anasikiza jaji huyo.

Shtaka lilisema alitoa hongo hiyo mnamo Januari 6, 2017 katika mahakama ya Milimani.

Mzee Joseph Wainaina akiwa mahakamani Julai 20, 2018. Picha/ Richard Munguti

Kabla ya jina lake kuitwa asimame kizimbani , Mzee Wainaina aliinama na kumwita wakili wake Bw Mbiyu Kama huku amejishika kichwa akisaga meno.

Mshtakiwa alimnong’onezea Bw Kamau jambo masikioni ndipo wakili huyo akaomba mahakama isimsomee mshtakiwa shtaka kwa vile anaugua.

“Naomba kesi dhidi ya Mzee Joseph Ngigi Wainaina ihairishwe kwa muda wa dakika kumi apate nafuu. Amenieleza hajisikii vizuri. Hata unaona anatokwa na jasho na anatetemeka,” wakili Mbiyu Kamau alimsihi hakimu mwanadamizi Bw Lawrence Mugambi.

Bw Mugambi aliahirishwa kesi hiyo na kuamuru mshtakiwa atolewe kizimbani apelekwe kwenye veranda akapate hewa safi.

Mzee Wainaina alitolewa nje na afisa wa pol;isi huku akitembea mwendo wa kinyonga.

Nje kwenye kiti kinachokaliwa na mashahidi wakisubiri kuingia mahakamani, Mzee Wainain alilia huku amejishika kichwa.

Alitoa pakiti ya tembe kwenye mfuko wa korti na kumeza huku akitokwa na jasho.

Alikaa kwa muda wa dakuika ishirini kisha akarudi ndani ya korti na kusomewa mashtaka mawili dhidi.

Shida ya kuugua kwa ghafla kwa , Mzee Wainaina ilianza aliposikia karani wa Jaji Aburili , Bi Adeline Shitawa Murunga akisomewa kuwa alipokea Sh50,000 kutoka kwake (mzee wainaina) amshawishi jaji atoe uuamuzi unaompendelea katika kesi nambari JR451/408/2016.

Mzee Wainaina na Bi Murunga walishtakiwa kila mmoja peke yake.

Karani huyo alishtakiwa kuwa mnamo Januari 6, 2017 katika mahakama kuu ya Milimani alipokea hongo ya Sh50,000 kutoka kwa Mzee Wainaina akidai atamshawishi Jaji Aburili atoa uamuzi unaompendeleza Mzee huyo.

Kila mmoja alikanusha mashtaka mawili na kuomba waachiliwe kwa dhamana.

“Mzee Maina amekuwa akifika katika afisi  za tume ya kupambana na ufisadi nchini, Hata leo (jana) alijisalamisha kwa mahakama. Alikuwa nje kwa dhamana ya Polisi ya Sh20,000,” alisema Bw Kamau.

Bw Mugambi aliamuru kila mmoja alipe dhamana ya Sh80,000 pesa tasilimu ama dhamana ya Sh200,000.

Kesi itatajwa tena Agosti 2, 2018 korti ielezwe ikiwa washtakiwa walipewa nakala za mashahidi.

You can share this post!

Akiri alipokea mamilioni kununulia wanakijiji shamba

Wakurugenzi 10 kortini kwa kufyonza mamilioni ya KPC

adminleo