Habari Mseto

Natembeya ajitetea kwa kufuta kazi wafanyakazi 700

Na EVANS JAOLA September 24th, 2024 1 min read

GAVANA wa Trans Nzoia George Natembeya ametetea kufuta kazi wafanyakazi 700 wa kaunti, hatua iliyozua maandamano.

Wiki jana, wafanyakazi katika idara mbalimbali walipigwa kalamu na kutakiwa kuwasilisha barua zao za ajira kwa uongozi wa kaunti ili kuthibitishwa.

Uamuzi huo uliibua maandamano huku waathiriwa wakishutumu kaunti kwa kuwafuta kinyume cha sheria.

“Nadhani walichochewa. Kuna maswali mazito ya ukaguzi kuhusu uajiri wao, na hatuwezi kuyapuuza,” Natembeya aliambia Taifa Leo.

Gavana Natembeya amewashutumu wafanyakazi hao kwa kutokuwa waaminifu, akisema kuwa walitakiwa kutoa barua za kuajiriwa lakini badala yake wakaandaa maandamano dhidi ya serikali yake.

“Nadhani walichochewa. Tunashughulikia suala hilo kwa ubinadamu zaidi. Kuna maswali mazito ya ukaguzi kutoka kwa ofisi ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu kuhusu uajiri wao, na hatuwezi kupuuza masuala haya,” Natembeya aliambia Taifa Leo.