• Nairobi
  • Last Updated May 16th, 2024 8:50 PM
Niligonga ng’ombe wala si kuua mwanamke ajalini – Dereva mlevi

Niligonga ng’ombe wala si kuua mwanamke ajalini – Dereva mlevi

Na STELLA CHERONO

Iwapo wasingepata nambari za usajiji za gari karibu na mwili wake, polisi wangechukulia mauaji ya Maureen Wambui Gachagua kama mengine yanayotekelezwa jijini na kukosa matumaini ya kuwapata washukiwa.

Hata hivyo, ilidaiwa kuwa mwanafunzi huyo wa mwaka wa tatu wa chuo kikuu cha Kenyatta, aligongwa na dereva mlevi kisha akaendesha gari lake kwa kilomita tatu mwili ukiwa juu ya gari hilo na kuutupa mtaani South C, Nairobi.

Maureen, 22, alikuwa akitoka kuhudhuria karamu akiwa na rafiki yake Dennis Mburu katika NextGen Mall kwenye barabara ya kuelekea Mombasa.

“Tulitoka NextGen Mall mwendo wa saa kumi Jumapili usiku. Nilifaulu kuvuka mtaro nje ya jumba hilo lakini rafiki yangu aliamua kufuata njia ya kufika barabarani. Nilimsubiri ili tuvuke barabara pamoja lakini alipofika kwenye lami, alianza kuvuka na nikaamua kumfuata kwa sababu barabara ilikuwa shwari. Kabla ya kufika upande wa pili, niliona gari likija kwa kasi na kumgonga,” alisema Dennis.

Alisema mwili wake ulitua juu ya paa la gari na akakimbia akitarajia ungeanguka ili ampeleke hospitalini.

“Lakini gari halikusimama, lilifululiza mwendo nikilifuata mbio hadi nikashindwa kulifikia. Nilijaribu kusimamisha magari mengine kwenye barabara ya Mombasa ili nilifuate lakini hayakusimama,” alisema.

Baada ya nusu saa aliacha kutafuta mwili na kurudi NextGen Mall, ambapo aliomba dereva wa teksi kumsaidia kumtafuta.

“Tulienda katika hospitali za Nairobi West, Nairobi South, Langata, Mater na Kenyatta lakini hatukumpata,” alisema.

Rafiki mmoja aliyempigia simu alimweleza kuna hospitali inayoitwa Mariakani. “Nilienda katika hospitali hiyo na nilipokuwa eneo la kupokea wageni nilisikia mwanamke akisema kuna mwili uliotupwa eneo hilo na mtu asiyejulikana,” alisema Dennis.

Alisema mwili ulikuwa katika hali mbaya bila miguu. Kando ya mwili kulikuwa na nambari za usajili za gari KCN 285B.

Polisi walipofika na umati kukusanyika mwendo wa saa kumi na mbili asubuhi, mtu alichukua nambari hizo na kutoweka.

Afisa anayechunguza ajali hiyo alisema Sajini Dismus Gitenge Motongwa wa idara ya magereza alipotupa mwili alielekea nyumba za makazi za askari wa gereza la wanawake la Langata, akaegesha gari, akang’oa nambari za nyuma za usajili na kuchukua gari tofauti.

Kisha alienda kituo cha polisi cha Langata na kuripoti kwamba aligonga ng’ombe kwenye barabara ya Langata.

You can share this post!

Wakuu wa Kenya Power walala ndani

Afueni kwa Waislamu tarehe ya kusafiri Mecca kusongeshwa

adminleo