• Nairobi
  • Last Updated May 8th, 2024 5:50 AM
Uhuru awapa vijana vyeo vya juu kuwatuliza

Uhuru awapa vijana vyeo vya juu kuwatuliza

Na PETER MBURU

RAIS Uhuru Kenyatta Jumanne alionekana kutaka kuwatuliza vijana ambao wamekuwa wakimkosoa kwa kuwapa wazee kazi, alipoteua vijana saba kuwa mawaziri wasaidizi (CAS).

“Ningependa Wakenya kutambua kuwa saba kati ya wale nimewapa kazi za manaibu waziri (CAS) ni vijana, wengine wa chini ya miaka 30. Natumai watafanya kazi na kujifunza kutoka kwa wenzao wenye uzoefu serikalini kwa lengo la kujiandaa kwa kazi za juu zaidi serikalini siku zijazo,” Rais Kenyatta akasema.

Hatua hiyo ni kufuatia malalamiko kutoka kwa vijana kuwa Rais Kenyatta anawapa kazi wazee waliostaafu huku maelfu ya vijana waliohitimu wakiwa hawana kazi.

Walioteuliwa kuwa Manaibu Waziri (CAS) ni Nadia Ahmed Abdalla na Maureen Magoma (Habari, Mawasiliano na Teknolojia), Ann Mukami Nyaga (Kilimo), Mumina Bonaya na Zacharia Kinuthia Mugure (Elimu), Abdul Bahari (Leba) na Lawrence Karanja (Viwanda).

Wengine ni Peter Odoyo (Ulinzi), Winnie Guchu (Afisi ya Sheria Serikalini), Wavinya Ndeti (Uchukuzi), Lina Chebii (Kilimo) na Mercy Mwangangi (Afya).

Vilevile, miongoni mwa Mawaziri Wasaidizi (CASs), Patrick Ole Ntutu alihamishwa kutoka Wizara ya Usalama wa Ndani hadi ya Leba, badala yake akiingizwa Hussein Dado ambaye alikuwa wizara ya Ugatuzi.

Rais pia alifanya mabadiliko miongoni mwa makatibu wa wizara, ambapo aliwateua Jwan Ouma kuwa katibu wa idara ya Mafunzo ya Kiufundi, Mary Kimonye (idara ya Huduma za Umma), Simon Nabukwesi (Masomo ya Vyuo vikuu na Utafiti), Solomon Kitungu (Uchukuzi), John Weru (Biashara) na Enosh Momanyi Onyango (Miundomsingi).

Baadhi ya makatibu waliohamishwa ni Joe Okudo (Utalii hadi Spoti), Kevit Desai (idara ya Mafunzo ya Kiufundi hadi wizara ya EAC), Kirimi Kaberia (wizara ya Spoti hadi ya Uchimbaji Madini), Esther Koimett (idara ya Uchukuzi hadi ya Utangazaji) na Colleta Suda (idara ya Masomo ya Vyuo Vikuu na Utafiti hadi idara ya Jinsia).

You can share this post!

Waziri Mkuu na mawaziri wote wa Urusi wajiuzulu

Uhuru atangaza mikakati kufufua kilimo Mlimani

adminleo