Habari Mseto

Upatanishi wasaidia kesi 600 kutatuliwa

July 30th, 2018 1 min read

Na MWANDISHI WETU

Mpango wa upatanishi uliozinduliwa na mahakama miaka miwili iliyopita, umesaidia kutatua kesi 600, Jaji Msimamizi wa Mahakama Kuu, Lydia Achode (pichani) amesema.

Alisema watu wengi wameanza kukumbatia mpango huo ambao kwa sasa umesaidia kutatua kesi hasa katika mahakama ya kututua mizozo ya kibiashara.

Akiongea katika kongamano la upatanishi la mwaka huu, Jaji Achode alisema mfumo huo unaendelea kukita mizizi katika mahakama.

Jaji Achode alisisitiza kuwa mfumo huo ni muhimu kwa kupunguza mrundiko wa kesi na kuachilia pesa zinazozimwa kwa sababu ya kesi.

Mahakama ilianza kufanyia majaribio mfumo huo Aprili 4 2016 katika mahakama ya kutatua mizozo ya kibiashara na ya kifamilia.

Baada ya mpango huo kufaulu katika vitengo hivyo, ulianza kutumiwa kutatua kesi za kijamii katika mahakama Kuu, Mahakama ya Watoto na Mahakama ya kutatua kesi za kibiashara.

Kwa sasa mipango ya kuanzisha upatanishi katika mahakama kote nchini umebuniwa na unaendelea kutekelezwa.