Waiguru aonya Mlima dhidi ya ‘kuhadaiwa’ kuunga mkono upinzani
GAVANA wa Kirinyaga Anne Waiguru amewataka watu kutoka Ukanda wa Mlima Kenya wasihadaike na kuupigia upinzani kura katika uchaguzi mkuu wa 2027.
Bi Waiguru anadai hakuna kiongozi wa upinzani ambaye ana uwezo wa kumshinda Rais William Ruto. Aliongeza kuwa upinzani umekosa mikakati ya kushinda uchaguzi mkuu na Rais Ruto atakuwa mamlakani kwa muda wa miaka 10.
Aliwakumbusha wakazi wa Mlima Kenya kuwa walikuwa na mkataba wa Rais Ruto kumuunga mkono mtangulizi wake Uhuru Kenyatta ahudumu miaka 10 kisha naye ahudumu kwa miaka 10.
Bi Waiguru alisema eneo hilo huenda likatengwa kisiasa iwapo halitamuunga mkono Rais Ruto.
“Ilikuwa miaka 10 ya Uhuru na miaka 10 ya Ruto. Tuhakikishe hatuendi kinyume cha makubaliano au muafaka huu kwa sababu tukiukiuka hata jamii nyingine hazitatuamini,” akasema Bi Waiguru.
Alikuwa akizungumza alipofungua wodi ya kujifungua kwa akina mama katika Kituo cha Kiafya cha Mutithi.
“Tulimpa Kibaki muda wa miaka 10 naye Uhuru miaka 10 kwa hivyo tumruhusu Ruto amalize miaka yake ili turejelee urais tena mnamo 2032. Tukikosa kumuunga Ruto basi hiyo itakuwa na maana kwamba tusubiri miaka 10 zaidi kabla ya kupata urais tena,” akaongeza Bi Waiguru.
“Maeneo mengine yanapambana ili kuwa serikalini na huwa nashangaa kwa nini baadhi ya watu wanataka tuingie upinzani ilhali tuko serikalini,” akasema.
Gavana huyo alifichua kuwa baada ya kukamilisha muhula wake wa miaka 10 analenga kuwakilisha eneo hilo kwenye wadhifa wa juu zaidi ambapo maamuzi yatakuwa yakifanya kuhusu mustakabali wa nchi.