Waliohodhi mahindi kuingia hasara baada ya shehena bei nafuu kuwasili kutoka Tanzania
WAKULIMA wa mahindi waliohodhi nafaka yao wakitarajia bei za juu huenda wakapata hasara huku bei zikikosa kubadilika sokoni, baada ya bidhaa za bei ya chini kuwasili kutoka mataifa wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na mavuno ya bidhaa za vyakula mbadala.
Katika eneo la Bonde la Ufa Kaskazini na maeneo mengineyo yanayokuza mahindi, bei zimeshuka kutoka Sh4,600 hadi Sh4,000 kwa kila mfuko wa kilogramu 90, na kusababisha hofu miongoni mwa wakulima kuhusu kuepuka hasara.
Karata ya wakulima inazidi kuwagharimu huku mifumo ya soko ikikosa kubadilika kuwafaidi.
Mahindi ya bei nafuu kutoka Tanzania yanayouzwa Sh3,700 kwa kila kilogramu 90, ongezeko la bidhaa mbadala kama vile viazi na mihogo, yamefurika sokoni.
Idadi kubwa ya wenye viwanda Bonde la Ufa Kaskazini wanauza kila gunia kati ya Sh4,000 na Sh4,100 huku bei ya shambani Moiben na Cherangany katika kaunti za Uasin Gishu na Trans Nzoia zikiwa Sh3,800.
Jumla ya trela 100 zilizopakiwa mahindi zinaingia nchini kupitia Isebania kutoka Tanzania kwa bei ya Sh3,700.
Data kutoka masoko eneo hilo inaashiria bei za mahindi hazijabadilika kwa kipindi cha mwezi mmoja uliopita na kuzima matumaini ya wakulima kuhusu ongezeko la bei baada ya kuvuna.
“Tulitarajia bei zipande baada ya kuvuna lakini hazijabadilika. Sasa tumekwama na mahindi kwenye mabohari na hatuna hiari ila kuuza kwa bei zilizopo sasa sokoni,” alisema James Songok, mkulima anayemiliki shamba kubwa kutoka Kerita, kaunti ya Uasin Gishu.
Kulingana na Wizara ya Kilimo, taifa lilizalisha mifuko 70 milioni ya mahindi msimu uliopita kutokana na mbolea ya bei nafuu ya serikali na hali shwari ya anga.