Habari

Ajabu mwanaharakati akisherehekea mwanawe kufungwa jela

Na ELVIS ONDIEK March 1st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SWALI ambalo wengi walijiuliza baada ya chapisho la Facebook mnamo Jumatano, kutoka kwa mwanaharakati wa kisiasa enzi za utawala wa Daniel Moi, Wafula Buke ni kwa nini baba asherehekee kifungo cha mwanawe gerezani.
Buke hakupongeza tu kifungo cha miaka minne alichokabidhiwa mwanawe Declan Neville na mahakama ya Kibera, bali pia alitamani kingekuwa ni miaka saba. “Kwa kuzingatia jinsi nilivyomjua, alifaa sana kwenda gerezani,” aliandika Buke, aliyekuwa mkurugenzi wa masuala ya kisiasa na mikakati katika Orange Democratic Movement (ODM).
Hata hivyo, kile ambacho hakusema katika chapisho lake ni kuwa mwanawe mwenye umri wa miaka 21 alikuwa amejiunga na kundi la uhalifu linaloratibiwa na maafisa wa polisi wasio waaminifu walio na mitandao Nairobi na maeneo mengine.
Buke aliambia Taifa Dijitali kuwa wanasajiliwa wanachama katika kundi hilo, wanashirikishwa katika ukaguzi mkali ikiwa ni pamoja na mbio, kama wale wanaojiunga na kitengo cha polisi.
“Mwanangu alichaguliwa kwa sababu ni mkimbiaji na ana mbio sana,” alisema, akiongeza kuwa Declan alikuwa na miaka 16 aliposajiliwa.
Anafikiri mwanawe alichukuliwa katika mitaa ya Kibera, Nairobi.
Mara tu akisajiliwa, wanachama wa kikundi hupatiwa silaha na ulinzi wanapofanya wizi, na mapato yanagawanywa miongoni mwao na maafisa wa polisi.
Buke alieleza kuwa siku moja, mwanawe alipigwa na umati baada ya wizi kutibuka huko Ngong na ni polisi waliomuokoa.
“Walimuokoa kutoka kifo kwa kuwa alikuwa mshirika wao,” alisema.
Buke, ambaye pia alikuwa kiongozi wa wanafunzi Chuo Kikuu cha Nairobi na alizuiliwa kwa miaka mitano chini ya Rais Daniel arap Moi, alisema hawezi kulinda mtu yeyote kutoka mikono ya sheria.
“Siliwalindi watoto wangu kutoka kwa ukweli,” alisema.
Alieleza jinsi alivyokuwa tayari mtoto wake mwingine atupe gerezani kwa kumpiga mke wake, na jinsi alivyokataa kulipia faini ndugu zake ili wafungwe jela kwa kuhusika na dawa za kulevya.
Kifungo cha mwanawe, alisema, ni fursa ya kumtoa kwenye mtandao wa uhalifu.
“Ni bahati sana alienda gerezani kwa sababu nilidhani alikuwa na mwezi au miwili tu kufa,” alisema Buke.
Buke pia alieleza historia ya mtoto wake akisema alizaliwa Kibera miaka 21 iliyopita katika familia maskini akikabiliwa changamoto za malezi na shule, na hatimaye akasajiliwa na maafisa wa polisi waliokuwa wakijihusisha na uhalifu.
Alieleza jinsi mwanawe alivyojaribu kujiondoa katika mtandao wa uhalifu lakini akijipata akiurudia tena.
Alisema kwamba kifungo cha miaka minne kinampa mwanawe nafasi ya kutafakari, kuwa salama, na kuandaa maisha mapya baada ya kutoka gerezani.
“Tunatarajia, akitoka nje, nitamtafutia sehemu salama ambapo anaweza kuanza maisha mapya,” Buke alisema.
Aliongeza kuwa majibu aliyoyapata baada ya chapisho lake la Facebook yamemshangaza, akipokea jumbe na simu nyingi kutoka kwa watu wanaokabiliana na tatizo sawa la watoto wao kuathiriwa na mitandao ya uhalifu.
Buke alieleza kwa kina kuhusu malezi ya mtoto wake, Declan, akisema alizaliwa katika mazingira magumu.
“Nilikuwa na maisha magumu sana wakati Declan alizaliwa. Nilikuwa nimetoka uhamishoni na sikuwa na mahali pa kuishi,” alisema.
Aliongeza kuwa, alijua kuwa mtoto wake alikulia katika mazingira yasiyokuwa na uthabiti na hakupata msaada wa kutosha.
“Mama yake alijua sikuwa na uwezo wa kumtunza, na akampeleka kwa mwanaume mwingine ambaye alijitolea kumlea,” alisema.
Alimshukuru mwanaume aliyekubali kumlea mtoto wake kama wake mwenyewe, ingawa baadaye aliondoka na kwenda Uganda, jambo ambalo lilifanya mama yake kurudi kwa Buke na kumwambia ukweli kuhusu mtoto wake.
“Nilifanya kipimo cha DNA, kilichothibitisha kuwa alikuwa mtoto wangu kwa asilimia 99.99,” alisema.
Buke alieleza kwamba alijitahidi kumsaidia mtoto wake kwa namna yote alivyoweza, lakini alikosa kuungwa mkono na mama wa Declan, ambaye aliishi na watoto wengine na alishindwa kumpa malezi bora.