Maswali tele watoto 4 waliotoweka Likoni wakipatikana wakitafuta kazi Tanzania
UCHUNGUZI umeanzishwa kubainisha jinsi wasichana wanne wa shule kutoka Likoni, Kaunti ya Mombasa, walivyoondoka nyumbani na kusafiri hadi nchi jirani ya Tanzania ambako walipatikana wakitafuta kazi.
Kulingana na wazazi wao, wasichana hao ni marafiki wa karibu na waliondoka nyumbani Jumatatu asubuhi ilivyo kawaida yao wakielekea shuleni, bila yeyote mwingine kufahamu mpango wao wa kutoroka.
Bi Mwanatumu Bakari, mzazi, alisema mtoto wake aliondoka nyumbani siku hiyo akiwa amebeba mkoba wake wa shule begani, lakini alishangaa jioni kugundua kuwa hakuenda shuleni kama alivyotarajia.
“Mtoto wangu aliondoka Jumatatu asubuhi na hajarejea nyumbani tangu wakati huo. Nilipowasiliana na mwalimu wake, aliniambia kuwa binti yangu hakufika shuleni,” alisema kwenye mahojiano Jumatano.
Bi Bakari baadaye alitafuta ushauri kwa mzazi mwingine na ndipo akagundua kuwa mtoto wa mzazi huyo pia alikuwa ametoweka.
Wanafunzi hao wanne wa Gredi 9 kutoka darasa moja wanadaiwa kupanga kwa makini mpango wao wa kutoroka.
Waliweka nguo na viatu ndani ya mikoba yao ya shule ili kuficha nia yao.
Mzazi mwingine, Bw Juma Swaleh, alisema baada ya kugundua kutoweka kwa mtoto wake, aliingia chumbani kwake na kukuta kabati lake likiwa tupu.
“Alikuwa amechukua vitu vyake vyote na kuacha vitabu. Hatukuona dalili yoyote wala hatukujua mipango yake ya kutoroka kwa sababu amekuwa akienda shuleni kila siku,” alisema.
Uchunguzi wa awali ulionyesha kuwa, wasichana hao walisimama kwa muda Diani, Kaunti ya Kwale, kwa shughuli isiyojulikana kabla ya kupanda basi kuelekea Tanzania.
Inasemekana walionekana Tanzania na mwanamke Mkenya aliyewahoji na baadaye kuripoti suala hilo kwa mzee wa kijiji katika nchi hiyo jirani.
Mzee wa kijiji aliwazuilia, na mmoja wao akatoa nambari ya simu ya wazazi wake.
Mzee huyo aliwapigia wazazi wao Jumatano asubuhi na kuwafahamisha hali hiyo, akithibitisha kuwa walipatikana wakiwa pamoja sokoni wakiomba kazi.
“Mzee wa kijiji alinipigia simu na nilifarijika kujua kuwa mtoto wangu yuko hai. Nilikuwa na hofu sana tangu alipotoweka bila kupokea taarifa yoyote kuhusu alipo,” aliongeza Bw Swaleh.
Hata hivyo, inashukiwa kuwa kuna mtu anayeendesha mtandao wa ajira haramu nchini Tanzania, akiwadanganya na kuwavutia wasichana wa shule kutoka Likoni kwa ahadi ya maisha bora.
Kulingana na mkazi wa eneo la Ujamaa, wasichana wengine wawili walirejeshwa nyumbani wiki mbili zilizopita baada ya kufuatiliwa na kupatikana nchini Tanzania.
“Hili sasa linaanza kuwa jambo la kawaida kwa sababu kuna matukio mengine mawili ambapo tulilazimika kuchangisha pesa ili kuwasaidia kurejea nyumbani baada ya kutoweka kwa siku kadhaa,” alisema Bi Amina Juma.
Wasichana hao wanatoka maeneo tofauti ya Likoni, yakiwemo Shika Adabu, Msikiti Punda, Mishi Mboko na Mwawechi.
Watatu wana umri wa miaka 16 na mmoja miaka 15.
Wazazi wao walioripoti tukio hilo katika Kituo cha Polisi cha Inuka, na badaye wakasafiri na polisi hadi Lunga Lunga kwenye mpaka wa Kenya na Tanzania ambako watoto hao walichukuliwa.
Duru katika idara ya polisi, ambao hawawezi kutajwa kwa kukosa mamlaka ya kuzungumzia suala hilo, walisema wasichana hao walikesha katika kituo cha polisi wakisubiri kuhojiwa Alhamisi kabla ya kukabidhiwa kwa wazazi wao.
Mahojiano hayo yanakusudia kusaidia uchunguzi mpana kuhusu uwezekano wa ulanguzi watoto.