Mradi kuimarisha maji safi Machakos, Konza City
Serikali inaongeza kasi ya utekelezaji wa mradi mkubwa wa miundombinu ya maji na majitaka katika eneo la Mashariki ya Chini, kwa lengo la kuboresha upatikanaji wa maji safi na huduma za usafi wa mazingira.
Jiji la Konza na mji wa Machakos ni miongoni mwa maeneo yatakayonufaika na mradi huo unaotekelezwa chini ya Mpango wa Maji na Usafi wa Mazingira Endelevu kwa Miji ya Kenya.
Awamu ya kwanza ya mradi ikikamilika inatarajiwa kuhudumia wakazi wasiopungua 150,000 katika mwaka wa kwanza, idadi inayokadiriwa kuongezeka hadi 330,000 kufikia mwaka 2040.
Mradi huo unasimamiwa na Shirika la Maendeleo ya Maji la Tana Athi (TAWDA) na unahudumia mji wa Machakos na maeneo ya jirani yakiwemo Muvuti, Kimutwa, Kiima Kimwe, Mumbuni, Katheka Kai, Mua na Mutituni.
Afisa Mkuu Mtendaji wa TAWDA, Sammy Naporos, alisema mradi umekamilika kwa asilimia 80.
“Shughuli zote zisizohusiana na Bwawa la Miwongoni, linalochangia takriban asilimia 20 ya kazi zilizosalia, zinatarajiwa kukabidhiwa kufikia Februari 13, 2026,” alisema wakati wa ziara ya ukaguzi Jumatatu.
Miundombinu iliyokamilika ni pamoja na Kiwanda cha Kutibu Maji cha Miwongoni, matangi matatu makubwa ya kuhifadhi maji katika Kiima Kimwe, Iveti na Katelembu, pamoja na kilomita 64.7 za mabomba ya kusafirisha na kusambaza maji.
Kupitia mradi huo visima vipya 11 vilivyo na vibanda vya kuuza maji vimechimbwa.
Bw Naporos alisema mpango huo umeimarisha zaidi usambazaji wa maji kwa familia, ukarabati wa mabomba ya zamani na ujenzi wa jengo jipya la ofisi za Kampuni ya Maji na Usafi wa Mazingira ya Machakos.
Hadi sasa,familia 1,500 zimeunganishwa na maji safi, huku idadi ikitarajiwa kuongezeka hadi takriban familia 330,000 kufikia 2040. Maji ya ziada yataelekezwa Konza City kusaidia yanayosambazwa kutoka Bwawa la Thwake na mradi wa Nolturesshi.
Ili kuboresha huduma za majitaka, ujenzi wa takriban kilomita 65 za mabomba makuu na ya matawi unaendelea katika mji wa Machakos na maeneo jirani. Aidha, kituo cha kutibu maji taka kinajengwa karibu na Mto Ikiwe kando ya Barabara ya Muvuti, na kitaendeshwa kwa nishati ya jua kupunguza gharama.
Hata hivyo, ujenzi wa Bwawa la Miwongoni ulicheleweshwa kutokana na changamoto za ardhi. Bw Naporos alisema suala hilo lilitatuliwa baada ya uamuzi wa mahakama kuunga mkono serikali mwishoni mwa mwaka jana.
“Tume ya Kitaifa ya Ardhi kwa sasa inashughulikia fidia ili kuruhusu ujenzi kuanza,” alisema.
Wakazi wamekaribisha mradi huo wakisema kuboreshwa kwa huduma za maji na usafi wa mazingira kutachochea ukuaji wa uchumi mijini na vijijini.
“Miradi hii ilipaswa kukamilishwa kitambo. Tunahimiza serikali iharakishe ili wananchi wanufaike,” alisema John Muya, mkazi wa Miwongoni.