Habari za Kaunti

Raia wa kigeni apigania mali baada ya ndoa yake na mkewe Mkenya kuvunjika

Na BRIAN OCHARO July 28th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RAIA wa Ireland aliyekuwa amehamia Kenya kwa matumaini ya kuanza maisha mapya na mwanamke aliyefahamiana naye kupitia mtandao sasa amejikuta akihusika katika kesi tatu mahakamani zinazohusu mamilioni ya pesa, mali na kuvunjika kwa ndoa yao.

Bw Joel Patrick Fitzpatrick anasema aliuza mali aliyorithi kutoka kwa marehemu mama yake nchini Ireland na kuhamia Watamu, Kaunti ya Kilifi, akiwa na hamu ya kuanzisha biashara na kujenga makazi pamoja na Bi Martha Wanjiru Muhoro, ambaye baadaye alifunga naye ndoa ya serikali mnamo Julai 23, 2025.

Hata hivyo, chini ya mwaka mmoja tangu ahamie Kenya, mwanajeshi huyo mstaafu wa Jeshi la Wanamaji la Marekani sasa anakabiliwa na kesi kadhaa, zikiwemo za madai kuhusu matumizi yasiyo halali ya urithi wake.

Katika kesi ya hivi punde iliyo mbele ya Mahakama ya Mazingira na Ardhi mjini Malindi, Bw Fitzpatrick anataka Mahakama imzuie Bi Muhoro kuuza, kuhamisha umiliki, kukodisha au kufanya shughuli yoyote kwa ardhi ya Gede/Dabaso, akidai ilinunuliwa kwa Sh25 milioni alizomtumia ili anunue kwa niaba yake.

Jumanne iliyopita, Mahakama ilimpa Bi Muhoro wiki mbili kuwasilisha majibu yake baada ya wakili wake kuomba muda zaidi.

Mahakama pia iliongeza amri ya kudumisha hali ilivyo na kuagiza pande zote mbili kubadilishana stakabadhi za kesi kabla ya kesi hiyo kutajwa Oktoba 12 kwa maelekezo zaidi.

Kulingana na stakabadhi za Mahakama, Fitzpatrick ni mshauri wa masuala ya biashara, siasa na mazingira.

Katika kesi nyingine ya madai, anaitaka Mahakama iamuru arejeshewe zaidi ya Sh35.8 milioni ambazo anadai alituma kwenye akaunti ya Benki ya Family inayomilikiwa na Bi Muhoro, huku akiomba akaunti hiyo izuiwe ili fedha zilizomo zisitolewe hadi kesi itakapoamuliwa.

Stakabadhi za Mahakama zinaonyesha kuwa wawili hao walifahamiana kupitia tovuti ya kutafuta wapenzi mwaka 2023.

Bw Fitzpatrick anasema alirithi asilimia 75 ya mali za marehemu mama yake, ikiwemo nyumba katika Kaunti ya Dublin nchini Ireland, na akamkabidhi Bi Muhoro jukumu la kuandaa uhamisho wake kwenda Kenya kwa kutafuta ardhi, kufuatilia taratibu za uhamiaji na kusimamia mipango ya kifedha.

Anadai alimtumia fedha nyingi, zikiwemo euro 250,000 (takriban Sh36.9 milioni) mwezi Aprili 2025 kwa ajili ya kununua ardhi na gari, pamoja na uhamisho mwingine wa euro 10,000 (takriban Sh1.5 milioni) mara nne, euro 15,000 (takriban Sh2.2 milioni) mwezi Septemba na euro 226,860 (takriban Sh33.4 milioni) mwezi Oktoba, ambazo anasema zilikuwa sehemu ya mwisho ya urithi wake.

Anadai Bi Muhoro alimshawishi fedha zote zipitie kwenye akaunti yake hadi atakapohamia Kenya, lakini baadaye hakumjumuisha katika umiliki wa ardhi na gari licha ya kuwa ndiye aliyefadhili ununuzi wake.

Bw Fitzpatrick anasema amebaki hana mali na ana hofu kuwa fedha zilizobaki zinaweza kutolewa kwenye akaunti hiyo kabla ya kesi kusikilizwa.

Kwa upande wake, Bi Muhoro anakiri kupokea fedha hizo lakini anakanusha kuzitumia vibaya.

Anasema matumizi yote yalifanywa kwa uwazi na kwa makubaliano ya pamoja walipokuwa wakijiandaa kuanza maisha yao ya ndoa.

Pia anasema aliacha kazi yake ya ualimu nchini Qatar kwa ombi la Fitzpatrick na kurejea Kenya kujiandaa kwa harusi yao.

Anaeleza kuwa mali hizo zilisajiliwa kwa jina lake kwa sababu wakati huo Fitzpatrick, akiwa raia wa kigeni, hakuwa na stakabadhi zilizohitajika kusajili mali hizo kwa jina lake.

Bi Muhoro anasema baadaye uhusiano wao ulivurugika na kumshutumu Bw Fitzpatrick kwa ukatili na unyanyasaji, akiiomba Mahakama itupilie mbali kesi hiyo.