Museveni asema ameshangazwa na ujanja wa Kenya
RAIS wa Uganda Yoweri Museveni amesema nchi yake ilisitisha ununuzi wa mafuta kupitia Kenya baada ya kugundua kile alichokitaja kuwa udanganyifu uliokuwa ukiigharimu mabilioni ya shilingi kupitia mabroka.
Akizungumza nchini Uganda, Museveni alisema mpango uliokuwa ukitumika haukuwa wa serikali kwa serikali (G2G) kama ulivyowasilishwa, bali ulikuwa mpango wa “serikali kwa mabroka”, ambapo Uganda ilinunua bidhaa za petroli kupitia mawakala waliokuwa wakinufaika kwa gharama ya walipa ushuru.
Uganda, ambayo haina bandari ya bahari, kwa muda mrefu imekuwa ikitegemea Bandari ya Mombasa na mtandao wa mabomba ya mafuta wa Kenya kuagiza mafuta yake.
“Kulikuwa na mawakala nchini Kenya waliokuwa wakiuzia Uganda mafuta. Hii ilikuwa janga kubwa. Sikujua hadi nilipoelezwa na seneta mmoja kutoka Kenya,” alisema Museveni.
Kulingana na rais huyo, alipopewa taarifa hizo aliwaagiza maafisa wake wa nishati kuchunguza suala hilo lakini hatua za haraka hazikuchukuliwa. Hata hivyo, baada ya uchunguzi zaidi, Uganda ilibadili mfumo wake wa ununuzi wa mafuta.
Kwa sasa Uganda inaagiza mafuta kupitia ushirikiano kati ya Kampuni ya Kitaifa ya Mafuta ya Uganda (UNOC) na kampuni ya Vitol, kufuatia mabadiliko ya sera yaliyofanywa mnamo 2023.
Museveni alisema hatua hiyo imepunguza kwa kiasi kikubwa gharama za mafuta. Kulingana na takwimu zilizotolewa na Katibu wa Wizara ya Nishati nchini Uganda, Irene Batebe, Uganda ilikuwa ikilipa wastani wa Sh15,340 kwa tani moja ya dizeli chini ya mfumo wa zamani, ikilinganishwa na Sh10,790 chini ya mfumo wa sasa.
Kwa petroli, gharama ilishuka kutoka Sh12,675 kwa tani moja hadi Sh7,995, huku gharama ya mafuta ya ndege ikishuka kutoka Sh14,853 hadi Sh10,303 kwa tani moja.
Aidha, serikali ya Rais William Ruto ilieleza kuwa mpango wa serikali kwa serikali (G2G) ulianzishwa mnamo 2023 ili kupunguza shinikizo la fedha za kigeni nchini.
Serikali ilisema sekta ya mafuta ilikuwa ikihitaji karibu Sh64.7 bilioni kwa mwezi fedha za kigeni kwa ajili ya uagizaji wa mafuta, hali ambayo ilikuwa ikitishia akiba ya fedha za kigeni na usalama wa nishati nchini.
“Sitasahau takwimu hizo. Zinathibitisha jinsi tulivyokuwa tukipunjwa kwa miaka mingi,” alisema Museveni.
Kauli yake imezua mjadala mkubwa nchini Kenya, hasa kutokana na jinsi serikali ya Rais William Ruto ilivyokuwa imewasilisha mpango wa G2G kama suluhu ya kupunguza shinikizo la fedha za kigeni na kuhakikisha upatikanaji wa mafuta nchini.
Hata hivyo, msemaji wa serikali ya Kenya Charles Owino alijibu kwa njia ya kidiplomasia akisema uhusiano kati ya Kenya na Uganda unaendelea kuwa mzuri.
“Tuna uhusiano mzuri wa kikazi na Uganda. Tunaendelea kushirikiana katika miradi mbalimbali ya miundombinu ya mafuta,” alisema Owino.
Wakati huo huo, aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua ameunga mkono madai ya Museveni akisisitiza kuwa mpango huo uliwanufaisha watu binafsi badala ya serikali ya Kenya.
Akizungumza katika mkutano nchini Amerika, Gachagua alidai kuwa biashara ya mafuta ni ya thamani ya mabilioni ya pesa na kwamba wanaonufaika ni watu walio ndani ya utawala wa Kenya Kwanza.
Kwa upande wake, mshauri wa rais wa masuala ya uchumi David Ndii alipinga madai hayo kupitia mtandao wa X, akisema kampuni zinazouzia Kenya mafuta zinamilikiwa na serikali husika, huku kampuni inayouzia Uganda ikiwa ya kibinafsi.
Mjadala huo umeendelea kuibua maswali kuhusu uwazi katika biashara ya mafuta na iwapo mfumo wa G2G uliokuwa ukitumika uliwanufaisha wananchi au mawakala.
Licha ya mvutano huo wa kisiasa, Kenya na Uganda zinaendelea kutegemeana kiuchumi, hasa katika sekta za biashara, usafirishaji na nishati, huku wadadisi wakisubiri kuona iwapo madai ya Museveni yatachochea uchunguzi zaidi kuhusu biashara ya mafuta katika eneo la Afrika Mashariki.