Habari za Kaunti

Ugonjwa wa Chikungunya: Dawa sasa kupulizwa mitaani

Na MISHI GONGO June 10th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

SERIKALI ya Kaunti ya Mombasa imeanzisha shughuli ya kunyunyiza dawa katika maeneo ya makazi na sehemu nyingine za umma ili kudhibiti maambukizi ya Chikungunya, homa ya dengue na malaria.

Hatua hiyo imechukuliwa baada ya mlipuko wa Chikungunya kuthibitishwa wiki iliyopita katika maeneo mbalimbali ya jiji hili la Pwani. Maafisa wa afya wameeleza kuwa, lengo ni kuwaangamiza mbu wanaoeneza ugonjwa huo.

Kulingana na maafisa wa afya, mbu aina ya Aedes wanaosambaza virusi vya Chikungunya hupatikana kwa wingi ndani ya nyumba, na hivyo kuwafanya kuwa hatari zaidi kwa wakazi.

“Hii ni kampeni ya kipekee inayolenga mbu wanaobaki na kuzaliana ndani ya nyumba. Tumeamua kupeleka vita hivi moja kwa moja hadi sehemu wanakotokea kwa wingi,” alisema afisa wa afya ya umma, Dkt Saumu Wayuwa.

Chikungunya ni ugonjwa wa virusi unaosababisha homa ya ghafla, maumivu makali ya viungo na misuli, upele, maumivu ya kichwa, na katika visa vichache, kutokwa damu.

Dalili huanza kuonekana kati ya siku mbili hadi saba baada ya kung’atwa na mbu.

Hakuna chanjo wala tiba ya Chikungunya. Wagonjwa wanashauriwa kupumzika, kunywa maji mengi, na kutumia dawa za kupunguza maumivu na joto mwilini.

Hata hivyo, dawa za makali ya kupunguza uchungu kama vile aspirin hazipendekezwi kutokana na hatari ya kutokwa damu kwenye viungo vya ndani ya mwili.

Wakati huo huo, Idara ya Afya ya Umma imetoa wito kwa wananchi kuchukua tahadhari za kibinafsi ikiwemo kwa kuvaa mavazi yanayofunika mwili, kulala ndani ya vyandarua vya kukinga mbu vilivyotiwa dawa, na kuondoa maji yaliyotuama karibu na nyumba zao.

“Chikungunya ni ugonjwa unaoweza kuzuilika iwapo kila mmoja wetu atachukua hatua zinazofaa. Ushirikiano wa jamii katika kampeni dhidi ya mbu ni muhimu sana kwa afya ya umma,” alisema Dkt Wayuwa.

Zoezi hilo la kunyunyizia dawa litaendelea katika wiki zijazo katika maeneo yote sita ya kaunti, hasa yale yaliyoathirika zaidi. Kaunti Ndogo zilizotambuliwa kuathirika zaidi ni Kisauni, Mvita, Nyali na Likoni.

Wakati uo huo, Serikali ya Kaunti imetoa wito kwa wakazi kushirikiana na maafisa wa afya wanaoendesha zoezi hilo na kuripoti visa vipya kwa vituo vya afya vilivyo karibu.

Kulingana na wataalamu, Mombasa hukumbwa na milipuko ya magonjwa yanayoenezwa na mbu kwa sababu ya ukosefu wa mifumo bora ya kuondoa majitaka, utupaji taka ovyo, na hali ya hewa inayotoa mandhari kwa mbu kuongezeka.