Walimu watishia kugoma kudai haki kwa Ojwang
Walimu katika Kaunti ya Kisumu wameapa kugoma kuanzia Jumatatu wakitaka Naibu Mkuu wa Polisi, Eliud Lagat, ajiuzulu kufuatia kifo cha mwalimu na mwanablogu Albert Ojwang’.
Chama cha Walimu wa Shule za Upili (KUPPET) tawi la Kisumu, kiliungana na familia ya Wakenya na familia ya marehemu kushinikiza kutiwa mbaroni kwa waliomuua mwalimu huyo akiwa mikononi mwa polisi.
Mwenyekiti wa KUPPET tawi la Kisumu, Bw Robert Onyando, alisema kuwa walimu wote watagoma kuanzia Jumatatu ikiwa serikali haitamchukulia hatua Bw Lagat, ambaye wanadai ni mshukiwa mkuu wa mauaji hayo.
“Tutafunga shule zote na hakutakuwa na masomo. Kuanzia Jumatatu, tutajitahidi kuhakikisha shule zote zimefungwa hadi haki itendeke,” Bw Onyando alisema.
Walimu hao waliandamana Ijumaa jioni hadi Kituo Kikuu cha Polisi cha Kisumu, kisha wakaelekea Uwanja wa Michezo wa Jaramogi Oginga Odinga ambapo walifanya ibada ya kuwasha mishumaa kwa heshima ya marehemu Ojwang’.
Katibu wa KUPPET Kaunti ya Kisumu, Bw Zablon Awange, alisisitiza kuwa Bw Lagat anapaswa kuchukuliwa kama mshukiwa wa moja kwa moja.
“Kusimamisha kazi maafisa sita wa chini wa polisi hakutoshi. Bw Lagat ndiye alilalamika dhidi ya Ojwang’, hivyo ni lazima ashtakiwe pia,” alisema Bw Awange.
Walimu pia walikemea msemaji wa polisi kwa kutoa taarifa za uongo kwamba marehemu alijiua.
Bw Awange alisema kuwa washukiwa wote wa mauaji hayo wanapaswa kuwekwa rumande ili wasiingilie mashahidi wa kesi hiyo.
“Hatutarudi nyuma hadi wauaji wa mwenzetu wakabiliwe na sheria. Tunawafundisha wanafunzi wetu kuwa Kenya ni nchi inayoongozwa na sheria kulingana na Katiba ya mwaka 2010,” akaongeza.
“Hatutaruhusu nchi yetu itumbukie katika hali ya uhalifu kama ilivyo Haiti kwa sasa.”
Walimu hao walisema kuwa kifo cha Bw Ojwang’ kinakiuka ahadi ya Rais William Ruto ya kumaliza visa vya utekaji nyara na mauaji ya kiholela.
“Ojwang’ alikamatwa mchana peupe kutoka nyumbani kwa wazazi wake, akasafirishwa hadi Nairobi na kuuawa ndani ya saa 24. Huu ni unyama wa hali ya juu zaidi kuwahi kushuhudiwa nchini,” alisema Bw Onyando.
Katika Kaunti ya Siaya, walimu walifanya ibada ya kuwasha mishumaa katika bustani ya Gavana wakiongozwa na Katibu wa KUPPET tawi la Siaya, Bw Sam Opondo.
“Tuko hapa kuomboleza mwalimu mwenzetu aliyepoteza maisha kwa njia ya kuhuzunisha. Alikuwa mwalimu mwenye bidii aliyekuwa na nafasi ya kubadilisha maisha ya wanafunzi wengi. Ni huzuni kwamba waliopaswa kumlinda ndio waliomuua,” akasema Bw Opondo.
Mwenyekiti wa tawi hilo, Bw Robert Ouko, aliwahimiza wananchi kuzungumza wazi na kutoogopa polisi.
Katika Kaunti ya Homa Bay, walimu walikutana nyumbani kwa wazazi wa marehemu, Bw Meshack Ojwang’, wakiongozwa na Katibu Mkuu wa KUPPET, Bw Akelo Misori, Katibu wa Tawi hilo, Bw Stephen Yogo, na Mwenyekiti Bw Jack Okoth.
Katika ibada hiyo ya usiku, ilibainika kuwa walimu wa eneo hilo wamekuwa wakilengwa na wahalifu mara kwa mara.
Bw Okoth alisema visa hivyo vimekuwa vikitokea asubuhi mapema au jioni wakati walimu wanatoka au kuelekea shuleni.
“Walimu wanaoshambuliwa ni wale wanaobeba vipakatalishi, simu au pesa taslimu. Wahalifu wanawalenga kwa urahisi. Polisi wachukue hatua kwani visa hivyo vimeripotiwa,” alisema Bw Okoth.
Walimu hao waliitaka serikali kutoa haki kwa familia ya Ojwang’ na kuhakikisha waliohusika wanakabiliwa vilivyo.
“Haki za walimu hazifai kupuuzwa. Tunastahili heshima kama Wakenya wengine,” aliongeza Bw Okoth.
Mjini Oyugis, wakazi wa Rachuonyo Kusini waliandamana barabarani Ijumaa wakiomba haki kwa familia ya marehemu Ojwang’. Walibeba mabango na picha za mwendazake wakililia haki itendeke.