Habari za Kitaifa

Acha kutumia polisi kunyamazisha wakosoaji wako, Karua na Mutunga waambia Ruto

Na KEVIN CHERUIYOT October 28th, 2024 Kusoma ni dakika: 2

KIONGOZI wa Narc Kenya Martha Karua na Jaji Mkuu wa zamani Willy Mutunga sasa wanadai kikosi haramu cha polisi ndicho kinahusika na msururu wa visa vya utekaji nyara wa wakosoaji wa serikali.

Wawili hao pia wamemsuta Rais William Ruto kwa kutumia polisi kunyamazisha wakosoaji wake.

Wakiongea na wanahabari Jumapili baada ya kukamatwa kwa mwanaharakati Boniface Mwangi, Bi Karua alidai kuwa wamepata habari za kuaminika kuhusu uwepo wa kikosi fulani eneo la Karen, Nairobi, ambacho wanachama wake huwateka nyara watu na kutoweka nao.

Alidai kuwa kikosi hicho kinashirikisha maafisa wa jeshi na idara ya polisi walioagizwa kulenga vijana wanaoelezea kuchukizwa na utawala wa Ruto.

“Visa hivyo wa utekaji nyara na mauaji ya kiholela ya watoto wetu, haswa vijana wasio na hatia, sasa ndio kitambulisho cha utawala wa Ruto,” Bi Karua akasema.

Kufuatia kukamatwa kwa Bw Mwangi akiwa nyumbani kwake kaunti ya Machakos, Bi Karua na Dkt Mutunga wametaka aachiliwe huru.

Wito sasa na huo pia ulitolewa na Waziri wa zamani Dkt Mukhisa Kituyi, Mkurugenzi wa Shirika la Kislamu za Kutetea Haki za Kibinadamu (MUHURI) Khelef Khalifa na aliyekuwa Mbunge wa Mukurweini Kabando wa Kabando.

“Tunataka haki za wanaharakati nchini ziheshiwe,” akasema Bi Karua.

Alidai kuwa Bw Mwangi alikamatwa na polisi wenye silaha ambao hawakujitambulisha kwake na kwa watu wa familia yake.

“Kenya haifai kuwa nchi ambayo familia zinaishi kwa hofu kwamba wapendwa wao wanaweza kuchukuliwa usiku na wasirejee nyumbani. Haki ya uhai iliyoko katika Katioba inapasa kuzingatiwa kikamilifu wala sio kwa masharti fulani,” Bi Karua akasema.

 Naye Bw Kabando akaongeza: “Tunahitaji uwazi kuhusu mahala walikozuiliwa wanaharakati hawa kulingana na Katiba ya Kenya na sheria ya kimataifa,” Bw Kabando akasema.

Baad ya kukamatwa nyumbani kwake Machakos, Bw Mwangi alizuiliwa katika Kituo cha Polisi cha Kamukunji Nairobi na atarajiwa kuwasilishwa kortini Jumatano kufunguliwa mashtaka ya uchochezi.

Rais wa Chama cha Mawili Nchini (LSK) Faith Odhiambo alithibitisha kuzuiliwa kwa mwanaharakati huyo katika kituo hicho cha polisi huku akiilaani serikali kwa utekaji nyara wa Wakenya wasio na hatia.

Imetafsiriwa na Charles Wasonga