Ayacko: Hatutaki viongozi wa Linda Mwananchi Migori
GAVANA wa Migori Ochilo Ayacko amewaonya viongozi wa kundi la Linda Mwananchi dhidi ya kuzuru kaunti hiyo, akisema ziara yao iliyopangwa inaweza kuongeza joto la kisiasa na kusababisha ghasia kama zile zilizoshuhudiwa hivi karibuni katika Kaunti ya Homa Bay.
Onyo hilo linatolewa wiki moja baada ya mapigano kati ya wafuasi wa ODM na kundi la Linda Mwananchi huko Homa Bay kusababisha vifo vya watu wawili na kujeruhi wengine kadhaa.
Kwa siku tatu zilizopita, Bw Ayacko amekuwa akitoa tahadhari kuhusu mpango wa Gavana wa Siaya James Orengo na viongozi wengine wa Linda Mwananchi kuzuru Migori kama sehemu ya kampeni zao katika eneo la Kusini mwa Nyanza.
Akizungumza wakati wa harambee katika Chuo cha Ualimu cha Migori, Gavana Ayacko alisema viongozi wa kisiasa wanafaa kushauriana na viongozi wa maeneo wanayonuia kuzuru, hasa pale ambapo kuna mvutano wa kisiasa.
Alisema ziara ya awali ya Bw Orengo mjini Homa Bay bila maelewano ya kutosha na viongozi wa eneo ilichangia mazingira yaliyozaa machafuko.
“Orengo alikuwa ameapa kufika Homa Bay hata iweje. Ziara yake bila mwaliko wa viongozi wa eneo na bila uungwaji mkono mashinani ndiyo chimbuko la matatizo yaliyoshuhudiwa,” akasema Bw Ayacko.
Gavana huyo aliwauliza waliohudhuria mkutano huo ikiwa wangependa Bw Orengo kuzuru Migori, huku wengi wakijibu kwa sauti kwamba hawamtaki.
Bw Orengo, Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino ni miongoni mwa viongozi wanaohusishwa na kampeni za Linda Mwananchi.
Bw Orengo ameashiria kuwa kundi hilo linapanga kuzuru maeneo mbalimbali ya Kusini mwa Nyanza, yakiwemo Migori na Homa Bay.
Katika ziara yao ya mwisho Homa Bay, viongozi hao walifanikiwa kuhutubia wakazi wa Nyandiwa na Sindo katika eneo la Suba Kusini.
Hata hivyo, mpango wa kufanya mkutano mjini Homa Bay ulivurugika baada ya kundi hilo kufika jioni na kukabiliwa na mapokezi baridi.
Machafuko yaliyofuatia yalisababisha kifo cha afisa mmoja wa polisi na mfanyabiashara mwanamke, huku mali ikiharibiwa.
“Jambo muhimu zaidi ni amani kudumu. Serikali yangu imejikita katika maendeleo, hasa kuboresha miundombinu ya barabara, na hatuwezi kuruhusu siasa kuvuruga amani,” akasema Bw Ayacko.
Wakati huo huo, Gavana wa Homa Bay Gladys Wanga amejitenga na madai yanayomhusisha na ghasia hizo na kutaka uchunguzi ufanywe dhidi ya wote watakaopatikana na hatia.
Aliyekuwa Naibu Gavana wa Homa Bay Oyugi Magwang ameonya kuwa kuendelea kwa vurugu za kisiasa kunaweza kutatiza juhudi za maendeleo kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.
Viongozi mbalimbali sasa wamewataka wanasiasa kushindana kwa sera na hoja badala ya kutumia ghasia, huku hofu ikiongezeka kuwa mivutano ya Homa Bay inaweza kusambaa hadi kaunti jirani za Nyanza.