Babu afariki katika mkanyangano akisubiri Sh200 kwa kuhudhuria mkutano wa Ruto
Mzee Ombui Orandi mwenye umri wa miaka 97 aliondoka nyumbani kwake kijiji cha Biyonge, Bomachoge Chache, Kaunti ya Kisii saa tatu asubuhi kuelekea kituo cha kibiashara cha Egetuki, umbali wa takribani kilomita tatu.
Licha ya umri wake mkubwa, Mzee Ombui alikuwa amezoea kufanya matembezi hayo kila siku kwenda kituoni na kurudi nyumbani
Hata hivyo, Jumatano, Aprili 15, 2026, ilikuwa tofauti kwake kwa kuwa mwanasiasa wake kipenzi, Rais William Ruto, alitarajiwa kufika katika kituo hicho.
Alikuwa na hamu kubwa ya kumuona, na alipokuwa akitembea aliwaambia watu kuwa alifurahi kwamba rais angefika “nyumbani kwao”.
Baada ya Rais kumaliza hotuba yake, kama ilivyo kawaida katika eneo la Gusii, wananchi walibaki nyuma kusubiri kupokea pesa (zinazojulikana kama Goserwa) kutoka kwa Mbunge wa eneo hilo Alpha Miruka.
Katika lango la KMTC Gucha, hali ilichafuka na mkanyagano mkali ukatokea. Dakika chache baadaye, mwili wa Mzee Ombui ulionekana umelala chini langoni.
“Rais alipoondoka, habari zilienea kwamba watu waende KMTC kupokea pesa. Baba yangu alikuwa na tatizo la kusikia, na alipofika langoni watu walianza kusukumana. Akaanguka na watu wakamkanyaga. Alikaa hapo kwa muda hadi ilipojulikana kulikuwa na mwili langoni ndipo mbunge akasitisha kugawa pesa,” alisema mwanawe, Joshua Ombui, akibainisha kuwa kila mtu alikuwa akipewa Sh200.
Familia hiyo ilisema baadaye ilipeleka mwili huo katika chumba cha kuhifadhi maiti cha Ogembo na kuanza mipango ya mazishi, ikieleza kuwa haina uwezo wa kifedha na inaomba msaada wa kumzika kwa heshima.
Tukio hilo liliripotiwa katika Kituo cha Polisi Ogembo saa sita na dakika 55 mchana chini ya OB No. 15/15/04/2026.
Mwana mwingine wa marehemu, Francis Nyabuto Ombui, alisema alimkuta baba yake asubuhi akielekea Egetuki na kumwambia kuwa alitaka kumuona Rais Ruto.
“Baadaye nilipokea simu kwamba baba yangu alikuwa amelala katika lango la KMTC,” alisema.
Aliongeza kuwa baba yao alipelekwa Hospitali ya Ogembo lakini juhudi za kumfufua hazikufua dafu.
Watu wengine kadhaa walijeruhiwa katika tukio hilo. Idadi kamili ya waliojeruhiwa haijathibitishwa, lakini Taifa Leo ilizungumza na mvulana wa darasa la tisa mwenye umri wa miaka 13 kutoka kijiji cha Kebere aliyepata majeraha ya kifua na mgongo.
Mama yake, Beatrice Barongo Ondieki, alisema alikuwa pia ameenda Egetuki kwa matumaini ya kupata pesa.
“Nilipata Sh200 na nikarudi. Baadaye nilipigiwa simu nikajulishwa mwanangu aliumia katika mkanyagano,” alisema.
Mbunge Alpha Miruka alieleza masikitiko yake kwa familia ya marehemu, akisema mkanyagano huo ulitokea mbali na eneo alilokuwa akigawa pesa.