Faili ya uchunguzi wa mlinzi wa Katibu Fikirini Jacobs yafungwa
MAHAKAMA ya Makadara imefunga faili ya uchunguzi dhidi ya mlinzi wa Katibu wa Masuala ya Vijana, Fikirini Jacobs kuhusu kupigwa risasi na kuuawa kwa kiongozi wa vijana mtaani Kariokor, Cecil Ouma, huku ikisubiri uamuzi wa Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP).
Mahakama ilisema faili hilo haiwezi kuendelea kuwa wazi kusubiri wachunguzi kukamilisha mchakato wa kuwasilisha ripoti ya uchunguzi wa kisayansi kwa Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma.
Afisa wa polisi, Rashid Charo alikamatwa kufuatia kifo cha Bw Ouma aliyepigwa risasi Juni 30 katika eneo la Kariokor, Nairobi, wakati wa hafla iliyohudhuriwa na Bw Fikirini Jacobs.
Baadaye aliachiliwa kwa dhamana ya Sh20,000 huku uchunguzi ukiendelea.
Katika kikao cha mahakama kilichoendeshwa kwa njia ya mtandao Jumatano, Hakimu James Juma Maiya alimkosoa afisa wa uchunguzi kwa kupotosha mahakama kuhusu hali ya kesi hiyo.
Katika kikao kilichotangulia siku 10 zilizopita, afisa huyo alikuwa ameambia mahakama kuwa faili ya uchunguzi tayari ilikuwa imewasilishwa kwa DPP na polisi walikuwa wakisubiri uamuzi wake.
Hata hivyo, ilibainika kuwa faili iliwasilishwa kwa DPP Agosti 18, siku moja tu kabla ya kikao cha Jumatano.
“Faili hii imefungwa. Afisa wa uchunguzi atasubiri maelekezo ya ODPP. Kwa sasa, faili imefungwa,” hakimu aliamuru.
Kufungwa kwa faili hakumaanishi kuwa suala hilo limefikia kikomo.
Sasa macho yote yako kwa DPP, ambaye atapitia matokeo ya uchunguzi wa kisayansi pamoja na faili ya uchunguzi kabla ya kuamua iwapo Bw Charo au mtu mwingine yeyote atafunguliwa mashtaka kutokana na kifo hicho.
Wakili wa Bw Charo, Cliff Ombeta, aliomba mahakama kumruhusu mteja wake kurejea kazini, akisema amezingatia masharti yote ya mahakama na amekuwa akihudhuria vikao kila alipohitajika.
“Hadi sasa, hajakuwa akienda kazini kwa sababu lazima aendelee kufuatilia hali hii,” alisema Bw Ombeta.
Wachunguzi wamekuwa wakitegemea kwa kiasi kikubwa ushahidi wa kisayansi kubaini aliyefyatua risasi iliyomuua Bw Ouma.
Polisi walipata bunduki mbili kutoka kwa walinzi wa Katibu huyo na kuziwasilisha kwa uchunguzi wa kitaalamu wa silaha.
Katika kikao kilichotangulia, wachunguzi waliambia mahakama kuwa matokeo ya uchunguzi huo yalikuwa tayari na faili ingewasilishwa kwa ODPP aipitie kabla ya hatua zaidi.
Bw Charo alikuwa miongoni mwa watu walioitwa kutoa taarifa kwa wachunguzi baada ya kubainika kuwa alikuwa ndani ya gari ambalo inadaiwa risasi ilifyatuliwa.
Uchunguzi wa mwili wa marehemu uliofanywa na madaktari waliowakilisha serikali na familia ya Bw Ouma ulionyesha kuwa alifariki kutokana na jeraha moja la risasi kifuani.
Madaktari walibaini kuwa risasi hiyo ilisababisha majeraha makubwa ndani ya mwili na akavuja damu kwa wingi ndani ya kifua, hali iliyosababisha kifo chake.
Uamuzi wa ofisi ya DPP utaamua iwapo uchunguzi huo utaishia kwa afisa huyo au mtu mwingine yeyote kufunguliwa mashtaka ya jinai kwa kuhusika na kifo cha Bw Ouma.