Habari za Kitaifa

Afisa wa polisi aliyeuawa Homa Bay alikuwa akisubiri kupandishwa cheo

Na DOMNIC OMBOK August 21st, 2026 Kusoma ni dakika: 1

KONSTABO Jim Richardson Onkundi, aliyefariki baada ya kupigwa na jiwe wakati wa mkutano wa Linda Mwananchi Homa Bay, alikuwa akisubiri kupandishwa cheo kuwa koplo.

Onkundi, 36, alikuwa akiendesha gari la polisi lililokuwa limewabeba maafisa watano kutoka Kituo cha Polisi cha Chemelil, Muhoroni, Kaunti ya Kisumu.

Alikuwa amemaliza mafunzo ya kupandishwa cheo katika Chuo cha Polisi Kiganjo na alikuwa akisubiri kuthibitishwa rasmi kabla ya kupewa cheo kipya.

Hata hivyo, ndoto yake ilikatizwa Jumapili baada ya jiwe kurushwa kwenye gari lao katika kituo cha kibiashara cha Olare walipokuwa wakirejea kutoka Homa Bay.

Jiwe hilo lilivunja kioo cha mbele na kumpiga Onkundi usoni na kichwani karibu na sikio la kulia.

“Aliyerusha jiwe alilenga gari letu moja kwa moja na kwa bahati mbaya jiwe lilimpata dereva. Alipoteza fahamu akiwa anaendesha,” alisema Kamanda wa Polisi wa Muhoroni Fredrick Ombaka.

Gari hilo aina ya Isuzu D-Max lilitoka barabarani na kugonga jengo baada ya Onkundi kupoteza fahamu.

Maafisa wengine waliokuwa ndani ya gari hilo pia walijeruhiwa.

Onkundi alipelekwa Jeneiro Hospital, Nyangeswo, kabla ya kuhamishiwa hospitali ya Rufaa na Mafunzo ya Jaramogi Oginga Odinga, Kisumu, ambako alitangazwa kufariki.

Afisa huyo alijiunga na polisi mwaka 2015 na alikuwa tegemeo la familia yake.

Ndugu yake Peter Onkundi alisema alizungumza na marehemu Jumapili asubuhi.

“Aliniambia alikuwa kazini Homa Bay na angenipigia simu baada ya kumaliza kazi. Hakupiga simu hiyo. Siku iliyofuata, mwenzake ndiye aliyenipigia na kunijulisha kuwa amefariki,” alisema.

Onkundi ameacha mjane na mtoto mmoja. Mwili wake ulihamishiwa mochari ya St Joseph’s Ombo Mission Hospital, Migori, huku mipango ya mazishi ikiendelea.

Afisa mmoja wa polisi alisema kifo cha Onkundi kinaonyesha hatari ambazo maafisa hukabili wanapotekeleza majukumu yao.

“Kila mtu ana haki ya kuishi, bila kujali taaluma yake au anatoka wapi,” alisema.

Alitoa wito kwa wananchi kushirikiana na polisi na kuepuka vurugu wakati wa mikutano ya kisiasa.