Habari za Kitaifa

Gavana Lenolkulal atozwa faini ya Sh84 milioni au asukumwe jela kula githeri

Na RICHARD MUNGUTI  August 29th, 2024 2 min read

ALIYEKUWA Gavana wa Samburu Moses Kasaine Lenolkulal ameweka historia kuwa afisa mkuu serikalini kufungwa kwa ufisadi.

Hakimu mkuu mahakama ya kuamua kesi za ufisadi Milimani Nairobi Thomas Nzioki, alimsukuma jela Bw Lenolkulal baada ya kumpata na hatia ya kupokea kwa njia ya ufisadi zaidi ya Sh83 milioni kwa kuuzia Kaunti ya Samburu mafuta ya petroli kati ya 2013 na 2019.

Mbali na kutozwa faini ya Sh85, 460, 995 ama atumikie kifungo cha miaka minane jela, Gavana huyo wa zamani na waliokuwa maafisa wakuu wa kaunti hiyo walizimwa kushikilia nyadhifa za umma kwa kipindi cha miaka 10, kuanzia Agosti 29, 2024.

Mfanya biashara Hesbon Ndathi aliyekuwa akisimamia kampuni ya Oryx Service Station alitozwa faini ya Sh83, 460, 995 kwa kujifaidi na pesa za umma.

Aliyekuwa afisa mkuu Stephen Letinina aliyeidhinisha kampuni ya Oryx ilipwe Sh83, 467, 995 alitozwa faini ya Sh1 milioni ama atumikie kifungo cha miaka minne.

Washtakiwa wote walijitetea wakisema walikuwa wanaugua na wameghairi matendo yao yaliyopelekea kaunti ya Samburu kupoteza kitita cha Sh83, 467, 995.

Lenolkulal kupitia kwa wakili Paul Nyamondi alisema atakata rufaa kupinga uamuzi huo.

Gavana huyo alipatikana na hatia ya kupokea kwa njia ya ufisadi kitita cha Sh83milioni miaka 11 iliyopita.

Bw Nzioki alisema makosa aliyofanya Lenolkulal ni kukataa kufichua kwamba kampuni ya kuuza mafuta ya Petroli ya Oryx Service Station ilikuwa yake.

Bw Nzioki alimpata na hatia gavana huyo aliyehudumu kwa miaka 10 katika mashtaka 10 na kumwachilia huru kwa kutumia vibaya mamlaka ya afisi yake.

“Baada ya kutathmini ushahidi wote, mahakama hii imewapata na hatia ya kushiriki ufisadi na kutumia vibaya mamlaka mliyokuwa nayo,” alisema Bw Nzioki akiwahukumu.

Lenolkulal na wenzake walipelekwa kuzuiliwa katika Gereza la Viwandani kuanza vifungo.

Walioshtakiwa kwa kutotunza pesa za umma ni Lenolkulal, Daniel Nakuo, Josephine Naamo, Reuben Marumben Lemunyete, Milton Lenolngenje, Paul Lolmingani, Bernard Lesurmat, Lilian Balanga na Geoffrey Barun.

Walitozwa faini ya Sh700, 000 kila mmoja ama watumikie kifungo cha miaka minne kila mmoja.

Kwa jumla, maafisa hao wanane waliokuwa wakuu wa zamani wa kaunti watalipa faini ya Sh5, 600, 000.

Pia, wafungwa hao hawatahudumu katika nyadhifa za umma kwa kushindwa kulinda na kutunza mali ya umma.

Shtaka lilisema washtakiwa walikula njama za kushiriki ufisadi kati Machi 27, 2013 na Machi 25, 2019 mjini Maralal, Kaunti ya Samburu kwa kulipa kampuni ya Oryx Sh83, 467, 995.

“Hii mahakama imefikia uamuzi kwamba upande wa mashtaka umethibitisha mashtaka 11 dhidi ya washtakiwa ya kushiriki ufisadi, kulipa kimakosa pesa za umma na kutumia vibaya mamlaka ya afisi,” alisema Bw Nzioki.

Wafungwa hao walitiwa pingu baada ya hakimu kusoma uamuzi huo saa mbili kasorobo usiku, Alhamisi, Agosti 29, 2024 na kupelekwa gerezani.

[email protected]