IEBC yaahidi mikakati kuzima wahuni vituoni wakati wa kuhesabu kura
TUME Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) imetangaza kuwa watu ambao si maajenti rasmi wa wagombeaji hawataruhusiwa kukaribia vituo vya kujumlisha kura ndani ya umbali wa mita 400 wakati wa uchaguzi mkuu ujao.
Kamishna wa IEBC Moses Alutalala alisema hatua hiyo inalenga kukomesha vitisho na vurugu ambavyo vimekuwa vikishuhudiwa katika chaguzi, akilaumu wanasiasa kwa kufadhili makundi ya wahuni.
Akizungumza mbele ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) inayoongozwa na Mbunge wa Butere Tindi Mwale, Bw Alutalala alisema tume itatekeleza kikamilifu sheria inayoruhusu IEBC kudhibiti shughuli zote ndani ya eneo la mita 400 kutoka vituo vya kujumlisha kura.
“Tutafanya kila tuwezalo ndani ya mita 400 ambazo kisheria ziko chini ya usimamizi wetu. Lakini nje ya hapo tunawaomba viongozi mtusaidie kwa sababu ni nyinyi mnaowaleta watu mnaowaita maajenti wakuu,” alisema.
Aliwalaumu viongozi wa kisiasa kwa kuwafadhili wahuni kisha kuilaumu IEBC baada ya kusababisha fujo.
“Wahuni wote wana wafadhili wao ambao ni viongozi wa kisiasa. Mkiacha kuwafadhili, tatizo la uhuni litakwisha,” alisema.
Kamishna huyo alisema IEBC ina wasiwasi mkubwa kuhusu ongezeko la makundi ya wahuni katika mikutano ya kisiasa na kwamba itatekeleza Kanuni za Maadili ya Uchaguzi bila upendeleo.
“Tuna kanuni ambazo kila mtu lazima afuate. Kama tume, tumeamua kuzitekeleza kwa usawa bila kujali mrengo wa kisiasa,” alisema.
Alifichua kuwa IEBC kwa sasa inabainisha maeneo yanayotajwa kuwa hatari kwa vurugu za kisiasa na itatoa taarifa hiyo baada ya kazi hiyo kukamilika.
Suala hilo liliibuliwa wakati makamishna wa IEBC walipofika mbele ya kamati hiyo kujibu hoja za Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kuhusu mwaka wa fedha wa 2021/2022.
Mbunge wa Teso Kusini Mary Emaase alitaka IEBC kuhakikisha ni maajenti rasmi wa wagombeaji pekee wanaoruhusiwa katika vituo vya kujumlisha kura ili kuzuia wahuni kuingilia uchaguzi.
Kwa upande wake, Mbunge wa Lugari Nabii Nabwera alishutumu IEBC kwa kutekeleza sheria kwa upendeleo akidai baadhi ya makundi ya kisiasa yanakosa kuchukuliwa hatua.
“Ukweli ni kwamba mnatumia sheria kwa upendeleo. Itumieni kwa usawa kwa wote ndipo tutakuwa na imani nanyi,” alisema.
Kauli hizo zinajiri huku ikisalia takriban miezi 13 kabla ya Uchaguzi Mkuu wa 2027 na visa vya wahuni wanaodaiwa kukodishwa na wanasiasa vikiongezeka katika mikutano ya kisiasa.
Tukio la hivi majuzi lilitokea Juni 14 katika Kanisa la All Saints, Nairobi, ambapo makundi ya vijana yalidaiwa kuwashambulia wanaharakati wa mashirika ya kiraia wakati wa mkutano wa kujadili bajeti.
Wakati huo huo, Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen amesema serikali haitavumilia watu wanaopanga vurugu.
Akizungumza mwishoni mwa wiki katika eneo la Mlima Elgon, alisema serikali imekabiliana na majangili, magaidi wa Al-Shabaab na sasa haitaruhusu wahuni kuvuruga amani ya nchi.
Pia aliwataka viongozi wa kisiasa kuhubiri uvumilivu, kukemea vurugu na kujadili masuala yanayowahusu wananchi badala ya kuchochea migawanyiko.