Kadhi Mkuu mpya hafai kutoka Pwani mara hii, wasema baadhi ya waislamu
SIKU chache baada ya mauti ya Kadhi Mkuu Sheikh Abdulhalim Hussein, viongozi wa Waislamu wameonyesha maoni kinzani iwapo mrithi wake anastahili kuendelea kutoka Pwani au ni wakati wa maeneo mengine kupata wadhifa huo.
Marehemu Hussein ambaye alikufa Julai 10 na kuzikwa siku hiyo hiyo alikuwa amehudumu katika wadhifa huo tangu Julai 2023. Alichukua wadhifa huo kutoka kwa Ahmed Muhdhar ambaye alistaafu baada ya kuwaongoza kwa miaka 12.
Bw Muhdhar alikuwa kadhi mkuu wa kwanza chini ya Katiba ya 2010 na alistaafu baada ya kutimiza umri wa miaka 60. Kumekuwa na kadhi sita tangu uhuru ambapo ni Abdalla Kassim kutoka familia ya Mazrui kisha nafasi yake ilichukuliwa na Swaleh Abdalla kutoka Zanzibar.
Alifuata Nassor Nahdy kutoka familia ya Nahdy Mombasa kisha Hammad Kassim kutoka familia ya Mazrui ambaye alimpisha Sheikh Muhdhar kisha Sheikh Abdulhalim, wote waliotoka Malindi.
Mchakato wa kumteua kadhi mkuu upo kwenye kifungo cha 170 cha Katiba na Sheria ya Mahakama za Kadhi. Kati ya masharti kwa anayelenga wadhifa huo ni kuwa na uzoefu wa miaka 15 ya mwalimu wa dini ya kiislamu.
Mauti ya Sheikh Abdulhalim, 55 ilikuwa mara ya kwanza ambapo kadhi mkuu alikuwa akiaga dunia akiwa afisini. Baadhi ya Waislamu sasa wanasema wadhifa huo sasa unastahili uendee nje ya Pwani hasa wakitaja kaskazini mwa kenya au maeneo mengine nje ya nchi.
Naibu kadhi mkuu Sukhyan Hassan alikiri kuwa kuna msukumo wadhifa huo uende nje ya Pwani lakini akasema suala hilo liko mikononi mwa Tume ya Huduma za Mahakama (JSC) ambayo ndiyo mwaajiriwa.
“Sheria inasema kuwa kunastahili kuwe na tangazo, mahojiano na mtu bora zaidi ateuliwe kadhi mkuu. Hata hivyo, baadhi wanauliza nafasi ya naibu kadhii mkuu ina maana gani kama hawezi kurithi nafasi hiyo jinsi ilivyo kwenye asasi nyingine za serikal,” akasema Bw Hassan anayetoka kaskazini mashariki kwenye mahojiano na Taifa Leo.
“Wadhifa huo haujetengewa eneo moja pekee ila maswali yameibuliwa iwapo kadhi mkuu atakuwa anatoka tu eneo moja, japo mwenyewe sitaki kujiingiza katika suala hilo,” akaongeza akisema kuna mahakama ya kadhi maeneo mengine nchini na si Pwani pekee.
Mwenyekiti wa Baraza la Waislamu Nchini (SUPKEM) Hassan Ole Naado alisema Katiba ya 2010 i wazi kuhusu uteuzi na mchakato wa urithi wa kadhi mkuu.
“Mwaajiri ni JSC na iwapo yeyote anahisi amefuzu basi atume maombi wadhifa huo ukitangazwa na wakiwa bora wataupata. Hata Sheikh Abdulhalim alipata wadhifa huo baada ya mchakato unaoeleweka kufuatwa,” akasema Bw Naado.
Imam wa Msikiti wa Mumias Sheikh Abbas Abdulaziz naye alipendekeza kadhi mkuu atoke nje ya Pwani kwa sababu kuna dhana kuwa wasiotoka huko hawathaminiwi kama Waislamu wa kweli.
“Kuna dhana wenye rangi fulani ndio wanajua dini kuliko sisi lakini hilo si kweli. Kwa hivyo, kuwa na kadhi mkuu kutoka nje ya Pwani itakuwa afadhali na itazima mianya hiyo ya migawanyiko,” akasema Sheikh Abdulaziz ambaye pia ni mwenyekiti wa Supkem tawi la Mumias.