Kesi kuhusu mauaji ya wapanga mikakati wa Ruto uchaguzi wa 2022 yasitishwa
MAHAKAMA Kuu jana ilizima kesi ya mauaji dhidi ya maafisa 15 wa usalama waliokuwa wakikabiliwa na mashtaka ya kuwateka na kuwaua raia wawili wa India na dereva wa teksi Mkenya kabla ya Uchaguzi Mkuu wa 2022.
Jaji Francis Olel alikubali ombi la Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP) Renson Ingonga la kusitisha kesi hiyo hatua iliyohitimisha mashtaka yaliyokuwa yamesubiriwa kwa zaidi ya miaka miwili.
Jaji Olel alisema DPP alitumia mamlaka aliyopewa na Katiba kwa njia halali.
“Nimebaini kuwa kuwasilishwa kwa ombi hili kulifanywa kwa mujibu wa sheria, kwa nia njema na kwa kuzingatia maslahi ya umma,” jaji alisema.
Hata hivyo, mahakama ilifafanua kuwa kuachiliwa kwa washukiwa hao hakumaanishi hawana hatia, wala hakuzuii kushtakiwa tena iwapo ushahidi mpya utapatikana.
Maafisa hao walitoka katika Kikosi Maalumu SSU kilichovunjwa, Idara ya Ujasusi wa Kitaifa (NIS) na shirika la KWS.