Maoni

MAONI: Umaskini usikushurutishe kukubali ‘Pesa za Damu’

Na DOUGLAS MUTUA September 17th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

HAKIKA, mnyonge hana haki. Hata ukimpa haki, anaweza kuikataa. Unyonge ninaorejelea hapa ni umaskini.

Mtu wa kipato cha chini atakuwa radhi kudharauliwa iwapo kufanyiwa hivyo kutampa hela.

Huwezi kunisadikisha vingine, hasa katika kisa ambapo mzazi ameuliwa mwana, halafu anaisihi mahakama imwonee imani muuaji kwa sababu muuaji mwenyewe, baada ya kuua, amemsaidia mzazi huyo kifedha.

Kisa cha wazazi wa marehemu Sharon Otieno – msichana aliyeuawa na aliyekuwa gavana wa Migori, Bw Okoth Obado – kuiomba mahakama impe adhabu rahisi, isiyokuwa ya kifungo gerezani, kisa na maana aliwasaidia baada ya kuua mtoto wao, kinaatua moyo.

Hakika, kinaudhi si haba unapozingatia kwamba msisitizo wa mahakama kuwa na imani unatarajiwa kumnufaisha Bw Obado pekee, si washtakiwa wenzake, Michael Oyamo na Caspal Obiero, ambao pia walikutwa na hatia ya kumuua Sharon.

Kumbe, kwa hakika, pesa ni mvunja mlima? Tofauti ya Bw Obado na washtakiwa wenzake ni pesa tu. Bw Oyamo na Bw Obiero, waliokuwa watu wa mkono wa Bw Obado, wanalazimika kusubiri uamuzi wa mahakama, hata ikiwa ni wa kunyongwa, kwa sababu hawana pesa.

Sina hakika Sharon mwenyewe angepewa fursa ya kuamua wanachopaswa kufanyiwa wauaji wake angesema aliye na pesa asazwe, maskini wasio na kitu waadhibiwe kwa vyovyote vile.

Huko ni kuutia hatiani umaskini.

Bila shaka watu watasema ni vyema kumsamehe aliyekukosea. Binafsi nakubaliana na mtazamo huo kwa asilimia zote. Msamaha unasisitizwa na imani na dini zote ninazojua. Hata hivyo, hakuna hata moja inayopendekeza kwamba aliye na pesa ahukumiwe tofauti na asiye nazo.

Mtazamo wa aina hiyo, na naandika haya kwa huruma na heshima zote wanazostahili wazazi wa Sharon, unamsawiri anayeupendekeza kama mtu aliye na uroho wa pesa.

Unamsadikisha tajiri kwamba, hata akimkosea maskini kwa kiasi gani, ilimradi ana uwezo wa kumfidia. hata nje ya mfumo wa mahakama, bado pesa zake zinaweza kumshawishi maskini akaghairi nia kuhusu adhabu kali anayostahili kupewa tajiri.

Kwa maoni yangu, kesi dhidi ya Bw Obado na wenzake ilisikilizwa yote mpaka hatua ya kutoa adhabu kwa sababu walishtakiwa na serikali, si wazazi wa Sharon.

Wazazi hao wangalipewa fursa ya kuiondoa, ili waelewane na wauaji hao nje ya mahakama, basi wangefidiwa kitambo sana mbali na macho yetu.

Kando na kwamba nawapa pole zangu wazazi hao, naamini hawajamtendea haki binti yao, pamoja na kilenge aliyeuawa kwa kuchomwa kisu akiwa bado tumboni mwa Sharon! Unyama ulioje!

Bila shaka, zamani jamii mbalimbali za Afrika zilikuwa na mifumo ya kuwapa haki waliotendewa unyama katika jamii. Baadhi zilipendekeza muuaji auawe, nyingine zikapendekeza alipe fidia ya ng’ombe, mbuzi, au kondoo wangapi …sijui! Aghalabu fidia ikilipwa na ukoo wa muuaji.

Hata hivyo, mfumo wetu wa mahakama ni wa kileo, tena haumruhusu muuaji na mwathiriwa kuketi chini ya mti na kupiga bei kuhusu damu ya aliyeuawa, kwa hivyo ilikuwa lazima kesi dhidi ya wauaji hao watatu ifuate mkondo mzima wa sheria.

Hali ingekuwa nyingine, wazazi wa Sharon wangalilaumiwa kwa kuipotezea mahakama muda na rasilmali muhimu ambazo zingetumika katika kesi nyingine kuwatafutia haki wanaostahili zaidi.

Kesi hiyo inanikumbusha kisa cha mwanahabari maarufu wa Saudia, Bw Jamal Khashoggi, ambaye aliuawa na serikali ya nchi hiyo katika ubalozi wake nchini Uturuki miaka kadha iliyopita, baadaye serikali hiyo-hiyo iliyomuua ikafidia familia yake kwa mamilioni ya pesa.

Familia hiyo ilichukiza wengi kwa kukubali hela hizo zinazoitwa ‘pesa za damu’ kutoka kwa serikali ambayo ilipanga mauaji ya mwenzao kwa kumchukulia kuwa mtu msumbufu, ikamuua kwa hakika, kisha ikaamua italipa fidia kiasi gani.

Maoni yangu ni kwamba, katika kisa ambapo umwagikaji damu umetokea, waathiriwa hawapaswi kuonyesha kwamba wanataka fidia ya pesa.

Mungu si maskini; hata ikiwa aliyeuawa ndiye aliyekukimu kifedha, kumbuka riziki hutoka kwa Mungu, hivyo atakupa kwa njia nyingine.

–       Douglas Mutua ni mwanahabari Mkenya anayeishi Amerika (mutua_muema@yahoo.com)