Habari za Kitaifa

Mahakama yazima ODM kumvua Sifuna wadhifa wake

Na BENSON MATHEKA February 12th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MAHAKAMA Kuu imezima kutimuliwa kwa Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna kama Katibu Mkuu wa ODM na ikazuia msajili wa vyama vya kisiasa kuchapisha kuondolewa kwake hadi kesi aliyowasilisha itakapoamuliwa.

Katika agizo lake, Mahakama Kuu ilisitisha utekelezaji wa maazimio ya kikao cha NEC ya ODM kilichofanyika Mombasa Jumatano ambacho tangazo la kumvua Sifuna wadhifa wake lilitolewa.

Katika kesi hiyo, Sifuna ameshtaki ODM na Msajili wa Vyama vya Kisiasa. Sifuna amekataa katakata uamuzi wa Kamati Kuu ya Kitaifa (NEC) ya Chama cha Orange Democratic Movement (ODM) wa kumng’oa katika wadhifa wa Katibu Mkuu, akisisitiza kuwa bado ndiye kiongozi halali aliyechaguliwa kushikilia wadhifa huo.

Akizungumza jijini Nairobi Alhamisi, Februari 12, 2026, Sifuna alisema hatua iliyochukuliwa na kikao cha NEC kilichofanyika Mombasa Jumatano ni kinyume cha katiba ya chama na inakiuka haki za kimsingi.

“Nimepokea tangazo lililotolewa na sehemu ya NEC kule Mombasa wakidai kuniondoa katika wadhifa wa Katibu Mkuu. Nataka kusema bila woga wowote kwamba hatua hiyo ni kinyume cha sheria, haikufuata taratibu na ni uvunjaji wa wazi wa Katiba ya ODM pamoja na kanuni za haki asilia,” alisema Sifuna.

Aliongeza: “Ninasalia kuwa mwanachama mwaminifu na Katibu Mkuu halali aliyechaguliwa na ODM. Nitaendelea kujitolea katika mapambano ya Kenya yenye haki, usawa na demokrasia.”

Uamuzi wa kumwondoa Sifuna ulitangazwa Jumatano baada ya kikao cha NEC Mombasa. Katika taarifa, chama kilisema baada ya kujadili mwenendo wa Sifuna, kiliazimia kumvua majukumu yake mara moja na kumteua Naibu Katibu Mkuu Catherine Omanyo kushikilia wadhifa huo kwa muda.

Hata hivyo, Sifuna amedai kuwa hakuwahi kupewa notisi ya tuhuma zozote wala kuitwa kujitetea.

“Hakuna wakati wowote nilijulishwa madai yoyote dhidi yangu, iwe ni utovu wa nidhamu au uzembe. Wala sijawahi kuitwa kujibu malalamishi yoyote,” alisema.