Mapanga 500 na silaha zingine zilisambaziwa wahuni Homa Bay, polisi wafichua
TAKRIBAN vijana 500 walilipwa kuziba barabara kuwazuia wafuasi wa Linda Mwananchi kuingia Homa Bay wakati wa mkutano wao Jumapili iliyopita, huku polisi wakifichua kuwa mapanga 500 na silaha nyingine zilisambazwa kabla ya ghasia hizo.
Ripoti ya kijasusi iliyotayarishwa baada ya polisi kunasa silaha hizo imeibua wasiwasi kuhusu kiwango cha maandalizi yaliyofanyika kabla ya mkutano wa Agosti 16.
Kamanda wa Upelelezi wa Jinai (DCI) wa Kaunti ya Homa Bay Jimmy Kisobo alisema polisi wanaendelea kuchunguza matukio yote yaliyotokea kabla, wakati na baada ya mkutano huo.
Alisema baadhi ya silaha zilisambazwa angalau siku moja kabla ya mkutano huo.
“Baadhi ya vijana si waaminifu kwa waliowafadhili kuzua vurugu. Wengine walioshiriki mapigano walishirikiana na maafisa na kutueleza idadi ya silaha zilizotolewa,” alisema Bw Kisobo.
Kulingana na polisi, uchunguzi umebaini kuwa hadi vijana 500 walihusika katika vurugu zilizotokea katika maeneo mbalimbali wafuasi wa Linda Mwananchi walipokuwa wakielekea Homa Bay.
Polisi pia wanachunguza matamshi ya baadhi ya viongozi wa Orange Democratic Movement (ODM) waliokuwa wameapa kumzuia Gavana wa Siaya James Orengo na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna kuingia Homa Bay.
Wakati huo huo, polisi walisema wafuasi wa Linda Mwananchi walikuwa wamechochea vijana kukabiliana na upinzani wowote ambao wangekutana nao njiani.
Maafisa wa usalama waliweka vizuizi kadhaa barabarani na kukagua magari yaliyokuwa yakielekea Homa Bay kabla ya mkutano huo. Operesheni hiyo ilisababisha polisi kunasa silaha na kuwakamata baadhi ya washukiwa.
Wakati wa mkutano huo, vijana wenye silaha kutoka pande mbili walikabiliana huku wanasiasa wakielekea katika maeneo mbalimbali ya mikutano.
Polisi walisema matukio kadhaa ya uhalifu yaliripotiwa kabla ya mkutano huo na baada ya wafuasi wa Linda Mwananchi kuondoka Homa Bay.
Maafisa katika eneo hilo walisema baadhi ya vijana wameanza kujitambulisha na wanasiasa fulani na mara nyingi hutoa ulinzi kwa viongozi wanaowaunga mkono wakati wa mikutano ya kisiasa.
Polisi walionya kuwa makundi kama hayo yanaweza kuhusika katika vurugu joto la kisiasa linapopanda.
Bw Kisobo pia alisema polisi wanamtafuta Khassim Abdi, ambaye amehusishwa na ghasia hizo na ambaye hakutii agizo la kujisalimisha.
Msemaji wa Huduma ya Kitaifa ya Polisi Muchiri Nyaga alisema Abdi aliamriwa kuripoti katika makao makuu ya DCI katika kaunti baada ya vurugu hizo.
Hata hivyo, kufikia Alhamisi hakuwa ametii wito huo, hali iliyosababisha mahakama kutoa kibali cha kukamatwa kwake.
Polisi pia wanachunguza uvamizi katika biashara mjini Homa Bay kabla ya mikutano hiyo.
Miongoni mwa zilizolengwa ni Homa Bay Tourist Hotel, ambako mali ya thamani ya zaidi ya Sh300 milioni iliharibiwa.
Washambuliaji waliingia hotelini wateja wakila na kuwalaumu kwa kutounga mkono serikali ya sasa.
Bw Kisobo alisema mtu aliyelengwa katika tukio hilo ni mwanasiasa anayewania kiti cha ubunge.
“Mwanasiasa huyo alijaribu kueleza kuwa anaunga mkono serikali na alikuwa ameonyesha nia ya kuwania kwa tiketi ya UDA. Lakini Abdi, ambaye pia anadai kuunga mkono tutam, hakutaka kusikia maelezo hayo,” alisema.
Mwanasiasa huyo, ambaye ana leseni ya kumiliki bunduki, alidaiwa kutoa bastola yake na kufyatua risasi hewani ili kuwatawanya vijana hao na kuzuia uharibifu zaidi.
Gavana wa Homa Bay Gladys Wanga, hata hivyo, alikanusha kuhusishwa na ghasia hizo.
“Hakuna tukio hata moja ambapo nimehusishwa na vurugu au ghasia katika kampeni zangu. Hatujawahi kufanya hivyo na hatuwezi kuanza sasa,” alisema.
Alisema hayo akitoa pole kwa familia ya Noreen Nalangwa, raia wa Uganda aliyefariki Jumapili baada ya kugongwa na gari lililokuwa likienda kwa kasi wakati wa vurugu zilizohusishwa na mkutano wa Linda Mwananchi.
Gavana huyo aliwataka vijana na wanasiasa waliotembelea eneo hilo kujizuia na kuepuka uchochezi.
Ghasia hizo zilisababisha vifo vya watu wawili na uharibifu wa mali, ikiwemo hoteli ya Homa Bay Tourist na ofisi za kanisa la Seventh Day Adventist (SDA).
Raia, polisi na wanahabari kadhaa walijeruhiwa, huku biashara katika baadhi ya maeneo ya Homa Bay Town zikifungwa kutokana na ghasia.