Habari za Kitaifa

Maraga alivyoshiriki maandano akiwa amevalia viatu spesheli

Na SAMMY WAWERU June 25th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

JAJI Mkuu mstaafu (CJ) David Maraga alikuwa miongoni mwa viongozi wakuu wa kisiasa waliojitokeza mnamo Jumatano, Juni 25, 2025 kushiriki maandamano ya kitaifa yaliyoongozwa na kizazi cha Gen Z.

Bw Maraga, ambaye tayari ametangaza nia kuwania kiti cha urais uchaguzi mkuu 2027, alijiunga na maandamano hayo ya vijana kupinga serikali, akiwa amevalia mavazi yaliyodokeza yuko tayari kusimama nao kidete, walipokabiliana na polisi wa kutuliza ghasia waliotumwa sehemu mbalimbali Jijini Nairobi.

Vijana wa Gen Z maeneo tofauti ya nchi, vile vile walishiriki maandamano, huku wakikabiliana vikali na maafisa wa polisi.

Jaji Mkuu wa zamani David Maraga alivyovalia wakati wa maandamano ya Gen Z mnamo Jumatano, Juni 25, 2025 Jijini Nairobi kukashifu ukatili wa polisi. Picha|Sammy Waweru

Aidha, wanapinga ukatili wa polisi, utekaji nyara na mauaji yanayotekelezwa na vyombo vya usalama.

Maandamano ya Jumatano pia yalikuwa kumbukumbu za mwaka mmoja tangu maandamano sawa na hayo kufanyika kote nchini, 2024, ambayo kwa mujibu wa mashirika ya kijamii, wanaharakati na mashirika ya kutetea haki za kibinadamu, yalisababisha vifo vya zaidi ya watu 60.

Akiwa amevalia koti la buluu iliyokolea na suruali ndefu aina ya jeans, Jaji Mkuu huyo wa zamani, CJ Maraga alionekana miongoni mwa waandamanaji akiwa amevalia viatu vya spesheli vya Skechers, ambavyo vinatambulika na wengi kufanya mazoezi kama vile kukimbia au kwenda kwenye mazoezi kusisimua misuli – gym.

Viatu aina ya Skechers alivyovalia CJ mstaafu David Maraga. Picha|Sammy Waweru

Bw Maraga alikuwa kati ya waandamanaji katika barabara ya Kimathi, kitovu mwa jiji la Nairobi (CBD), ambapo, majira ya saa tano kasorobo asubuhi, polisi waliporusha gesi ya vitoza machozi alikokuwa alilazimika – yeye na wengine kukimbilia katika ofisi za Nation Media Group kutafuta hifadhi ya muda.

Shingoni, Bw Maraga alikuwa amejifunga skafu yenye rangi na nembo ya bendera ya Kenya, ishara ambayo imekuwa ikitumiwa na vijana wa Gen Z kukumbuka waliopoteza maisha yao wakati wa maandamano ya mwaka jana.

Akiwa kwenye jengo la Nation, Rais huyo wa zamanai wa Idara ya Mahakama alionekana akiinama kufunga kamba za viatu vyake.

Upekuzi wa Taifa Leo kwenye majukwaa kadhaa ya ununuzi mitandaoni, ikiwemo Designer Outlet Stores (DOS), umebaini kuwa jozi moja ya viatu vya Skechers huuzwa hadi Sh19,900.

CJ Maraga alikuwa miongoni mwa viongozi kadhaa wa upinzani na wanaharakati wa haki za kibinadamu walioshiriki maandamano ya Jumatano dhidi ya ukatili wa polisi.

Shingoni, Bw David Maraga alikuwa amejifunga skafu yenye rangi na nembo ya bendera ya Kenya, ishara ambayo imekuwa ikitumiwa na vijana wa Gen Z kukumbuka waliopoteza maisha yao wakati wa maandamano ya mwaka jana, 2024. Picha|Sammy Waweru

Kinyume na madai ya polisi, alisisitiza kwamba waandamanaji walikuwa watulivu.

“Ninachoshuhudia ni waandamanaji waliojitokeza wakiwa na amani. Ninachowaambia, na nitaendelea kuwaambia ni kuwa tufanye maandamano kwa njia ya amani. Hicho ndicho kitu cha muhimu,” Bw Maraga aliambia waandishi wa habari nje ya jengo la Nation.

Tangu atangaze hadharani nia yake kutaka kumrithi Rais William Ruto mwaka 2027, CJ Maraga amekuwa ameelezea kusikitishwa kwake na ukatili wa polisi na ukiukwaji wa haki za kibinadamu.

Aidha, anasisitiza haja ya serikali kuheshimu utawala wa sheria na kulinda utu wa binadamu.

Akieleza sababu ya kushiriki kwake maandamano ya Jumatano, alisema, “Tunataka Katiba iheshimiwe. Tunataka maisha ya binadamu yathaminiwe.”

Maraga alisema, mbali na kuona waandamanaji waliojitokeza kwa wingi kwa amani hakushuhudia vurugu zozote kama inavyodaiwa na vyombo vya kushika doria.

Aliyekuwa Jaji Mkuu, CJ David Maraga akifunga kamba za viatu vyake kwenye jengo la Nation Media Group, Nairobi. Picha|Sammy Waweru

Idara ya Polisi (NPS) imejipata kwenye kikaango moto hasa kufuatia kifo cha mwalimu na mwanablogu Albert Ojwang’ akiwa kwenye seli ya polisi, tukio la kikatili lililoibua hasira kwa Wakenya.

Maafisa kadhaa, wakiwemo Mkuu (OCS) wa Kituo cha Polisi cha Nairobi ya Kati, Samson Taalam, na naibu wake Samuel Ng’ang’a, mshukiwa mkuu wa mauaji hayo — Konstebo James Mukhwana, pamoja na raia kadhaa tayari wamekamatwa huku uchunguzi ukiendelea.

Wakiendelea kuzuiliwa, washukiwa hao wamefikishwa mahakamani huku wito ukizidi kutolewa wa kukamatwa kwa Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi (Kitengo cha Polisi wa Kawaida), Eliud Lagat, ambaye hivi majuzi alitangaza kujiondoa kwa muda kwenye ofisi ya hadhi ya juu anayoshikilia ili kuruhusu uchunguzi kufanyika.

Lagat, ambaye bado yuko kikosini, ametajwa kuhusika na kifo cha Ojwang’, kwani anadaiwa kuagiza maafisa wa Idara ya Upelelezi wa Jinai na Uhalifu (DCI) kumkamata bloga huyo nyumbani kwake, Kaunti ya Homa Bay.

Waandamanaji kwenye barabara ya Kimathi, Nairobi. Picha|Sammy Waweru