Habari za Kitaifa

Maraga ampa Ruto siku saba achapishe ripoti iliyopendekeza mageuzi ya polisi lau sivyo aitoe yeye

Na DANIEL OGETTA August 19th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

ALIYEKUWA Jaji Mkuu David Maraga amempa Rais William Ruto muda wa siku saba kuchapisha ripoti ya jopo la marekebisho ya polisi iliyowasilishwa kwake mnamo 2023, akionya kwamba asipofanya hivyo ataichapisha mwenyewe.

Maraga, ambaye alikuwa mwenyekiti wa jopo hilo, alisema mojawapo ya mapendekezo makuu katika ripoti hiyo ilikuwa kurejesha uhuru wa Huduma ya Kitaifa ya Polisi (NPS) ili kuzuia kile alichokitaja kama kutekwa, kutumiwa vibaya na kuingiliwa kwa taasisi hiyo.

“Kwa kuwa ripoti hii iliandaliwa kwa gharama ya umma na kwa mujibu wa Kifungu cha 35 cha Katiba, ninakutaka uichapishe mara moja na bila kuhaririwa ndani ya siku saba. Usipofanya hivyo, nitaitoa mimi mwenyewe,” alisema Maraga.

Alisisitiza kuwa NPS ni huduma huru ya usalama wa taifa ambayo haipaswi kupewa maagizo na mtu yeyote, ikiwemo Rais, katika kutekeleza majukumu yake ya kikatiba.

Hata hivyo, Maraga alisema hivi majuzi nchi imeshuhudia kile alichokiita “ghasia za kisiasa zilizopangwa, matumizi ya magenge ya wahuni na upendeleo wa polisi” katika maeneo ya Homa Bay, Keumbu na Ol Kalou, pamoja na matukio ya vurugu katika makanisa ya Kisumu, Nairobi na Witima.

Homa Bay ilikumbwa na vurugu Jumapili wakati mkutano wa kisiasa wa Linda Mwananchi ulipovurugwa, ambapo watu wawili, akiwemo afisa wa polisi, waliuawa huku wengine 46 wakijeruhiwa.

Kulingana na Maraga, matukio hayo yaliyotokea chini ya utawala wa Rais Ruto yanaashiria kurejea kwa siasa za ghasia na matumizi ya idara za usalama kuzima sauti za wanaopinga serikali.

“Hii ni njia ambayo nchi iliwahi kupitia hapo awali kwa gharama kubwa. Haipaswi kuirudia tena,” alisema mgombea huyo wa urais wa chama cha United Green Movement (UGM), akihusisha hali hiyo na kile alichokiita “kutekwa kwa Huduma ya Kitaifa ya Polisi.”