Habari za Kitaifa

Linda Mwananchi waapa kuchukua hatua za kisheria na kiraia kukabili serikali kuhusu uhuni

Na JUSTUS OCHIENG, KEVIN CHERUIYOT August 19th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

VUGUVUGU la Linda Mwananchi limetangaza mkakati wa kukabiliana na kile inachodai ni ongezeko la ghasia za kisiasa nchini.

Mkakati huo unahusisha hatua kali za kisheria mahakamani, kushinikiza idara za usalama, uasi wa kiraia na kuhamasisha zaidi mashirika ya kiraia pamoja na vyombo vya habari.

Kundi hilo limesema hatua hizo zitachukuliwa kufuatia vurugu zilizovuruga ziara yake katika Kaunti ya Homa Bay Jumapili iliyopita, ambapo watu walifariki dunia, makumi kujeruhiwa na mali kuharibiwa.

Badala ya kujiondoa kwenye shughuli za kisiasa, viongozi wa Linda Mwananchi wanasema tukio la Homa Bay limeimarisha azma yao ya kupinga kile wanachokiita ghasia na vitisho vinavyofadhiliwa na serikali.

Kundi hilo linasema kwa sasa litafuata njia za kisheria, lakini limeonya kuwa huenda likalazimika kutumia hatua za kiraia ikiwa serikali haitawawajibisha waliohusika na vurugu hizo.

Gavana wa Siaya, James Orengo, ambaye ni mmoja wa viongozi wa vuguvugu hilo, alisema Jumanne kuwa yuko tayari kukabiliana na kile alichokiita “ugaidi wa serikali” na akashutumu serikali ya Rais William Ruto kwa kupanga mashambulizi dhidi ya wapinzani wa kisiasa.

“Tuko tayari. Niko tayari kukabiliana na changamoto yoyote inayotokana na ghasia za serikali. Huu ni ugaidi wa serikali unaoendelezwa na Rais William Ruto na lazima awajibike,” alisema Bw Orengo nje ya makao makuu ya Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) katika Barabara ya Kiambu, Nairobi.

Alikuwa amemsindikiza Bw Oliver Jaoko, maarufu kama Olivetti, ambaye polisi wanamtafuta kuhusiana na vurugu zilizoshuhudiwa katika mkutano wa Linda Mwananchi mjini Homa Bay.

Bw Orengo pia alishutumu serikali kwa kuandaa mazingira ya kuahirisha Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2027, ingawaje hakutoa ushahidi wowote kuhusiana na madai hayo.

“Rais Ruto anajaribu kutuandaa kuahirisha uchaguzi. Hilo halitawezekana,” alisema.

Kundi hilo limetaja maeneo manne ya mkakati wake: mahakama, maandamano na uasi wa kiraia, kushinikiza polisi na vyombo vingine vya usalama, na kuhamasisha mashirika ya kiraia na wanahabari kufuatilia shughuli zake moja kwa moja.

Njia ya kwanza ni kupitia mahakama. Katika taarifa yake ya Jumatatu, Linda Mwananchi lilisema litashinikiza uwajibikaji kupitia Katiba, mahakama na taasisi nyingine za kisheria.

“Kila mhuni na afisa ambaye sura yake ilinaswa kwenye kamera akihusika katika vurugu hizi, alionekana na anatambulika,” kundi hilo lilisema.

“Tutatumia Katiba, mahakama na taasisi zote za kisheria kuhakikisha kuna uwajibikaji.”

Pia limetaka Huduma ya Kitaifa ya Polisi (NPS), Mamlaka Huru ya Kusimamia Polisi (IPOA) na Idara ya Kitaifa ya Ujasusi (NIS) zifanye uchunguzi kuhusu mwenendo wa maafisa wao wakati wa vurugu za Homa Bay.

Linda Mwananchi linadai maafisa wa usalama walitazama tu huku wafuasi wake wakishambuliwa au walisaidia kuvuruga shughuli zake za kisiasa.

Madai hayo hayajathibitishwa kwa njia huru na vyombo vya usalama bado havijayakubali hadharani.

Kundi hilo linadai msafara wake ulikumbana na vizuizi vya barabarani tangu mpaka wa Kisumu na Homa Bay, na kuendelea kukabiliwa na vizuizi ndani ya kaunti hiyo.

Linaongeza kuwa watu wenye silaha waliokuwa wamejipanga kando ya barabara walifyatulia risasi msafara huo.

Moja ya madai makubwa zaidi yanahusu mtu aliyekamatwa na wafuasi wake Nyandiwa ambaye alidaiwa kujitambulisha kama afisa wa NIS.

Kundi hilo linasema simu yake ilichukuliwa na baadaye watu waliojieleza kuwa maafisa wakuu wa polisi waliwasiliana wakitaka irejeshwe.

Nguzo ya pili ya mkakati huo ni shinikizo la kisiasa kupitia maandamano na uwezekano wa uasi wa kiraia.

Seneta wa Vihiga, Godfrey Osotsi, alisema kundi hilo linaweza kuchukua hatua za kiraia iwapo Rais Ruto ataendelea kudumisha serikalini maafisa wanaotuhumiwa kupanga ghasia za kisiasa.

“Tutarejea kwenye hatua za kiraia ikiwa Ruto ataendelea kuwaweka watu hawa serikalini,” alisema Seneta Osotsi.

Nguzo ya tatu ni kishinikiza polisi moja kwa moja.

Orengo na Mbunge wa Embakasi Mashariki, Babu Owino, walimsindikiza Jaoko kwenda kujisalimisha kufuatia maslahi ya polisi katika uchunguzi wa vurugu hizo.

Bw Owino alishutumu polisi kwa kushindwa kuchukua hatua wakati timu ya Linda Mwananchi ilishambuliwa Homa Bay, akisema walipaswa kurejesha utulivu na kulinda wananchi.