Habari

Satelaiti kuziba pengo la intaneti mashinani

September 9th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

KWA mwanafunzi aliye kijijini, kukosa intaneti humaanisha kukosa kusama mtandaoni.

Kwa mgonjwa, kunaweza kumaanisha kusubiri hadi afike hospitalini ili kupata ushauri wa daktari.

Kwa mwananchi wa kawaida, huduma inayopatikana kwa simu au mtandao inaweza kumlazimu kusafiri kilomita kadhaa hadi mjini kwa sababu eneo analoishi halina intaneti.

Hata hivyo, hali hiyo inaweza kubadilika kwa matumizi ya intaneti ya satelaiti, ambayo inalenga kufikisha mawasiliano katika maeneo ambayo minara na nyaya za kawaida za intaneti hazijafika.

Kampuni ya Paratus Kenya, kwa ushirikiano na Starlink, imeanza kusambaza huduma hiyo katika maeneo ya mbali na ambayo hayajahudumiwa ipasavyo nchini.

Teknolojia hiyo inajaribiwa katika sekta kama afya na elimu, ambako intaneti si anasa tena bali imekuwa sehemu muhimu ya kupata huduma.

Akizungumza jijini Nairobi, Mkurugenzi Mkuu wa Paratus Kenya, Joseph Kibiwott, alisema kampuni hiyo inatafuta njia za kuhakikisha watu wanaoishi mbali na miji hawaachwi nyuma.

“Tunatafuta namna ya kupanua muunganisho wa intaneti katika maeneo ambayo hayajahudumiwa ipasavyo nchini,” alisema Kibiwott.

Kaunti ya Murang’a ni miongoni mwa maeneo ambayo teknolojia hiyo inafanyiwa majaribio.

Gavana Irungu Kang’ata alisema intaneti ya satelaiti tayari imetumika katika huduma za afya, ikiwemo telemedicine, inayowawezesha wagonjwa kupata ushauri wa kimatibabu bila kulazimika kusafiri hadi vituoni.

“Tumetumia teknolojia hii katika maeneo kama telemedicine na tunaangalia pia jinsi inavyoweza kutumika kwenye magari ya wagonjwa,” alisema.

Hii ina maana kwamba ambulensi njiani, wahudumu wanaweza kuwa na uwezo wa kuwasiliana na wataalamu wa afya na kupata usaidizi kwa wakati unaofaa.

Kang’ata pia alisema matumizi ya teknolojia hiyo yamesaidia baadhi ya idara za kaunti kupunguza gharama za intaneti.

Hatua hiyo inakuja wakati huduma nyingi muhimu, kuanzia elimu na afya hadi huduma za serikali na biashara, zikihamia mtandaoni.

Kampuni hiyo sasa inalenga kupanua mfumo huo katika nchi nyingine za Afrika Mashariki.