Matiang’i aacha kazi ng’ambo kuja kuwania urais nchini 2027
ALIYEKUWA Waziri wa Usalama wa Ndani Dkt Fred Matiang’í amepeana notisi ya kuacha kazi katika Benki ya Dunia ili kurejea nchini na kuanza kampeni ya urais wa uchaguzi mkuu wa 2027.
Dkt Matiangí anapanga kuwania uongozi wa nchi kwenye uchaguzi mkuu wa 2027 dhidi ya Rais William Ruto ambaye atakuwa akisaka muhula wa pili.
Mnamo Alhamisi, sekretariati ya kampeni ya Dkt Matiang’i ilithibitisha kuwa waziri huyo wa zamani, amepeana notisi ya miezi mitatu ili kujiuzulu kutoka kwa kazi yake hiyo na Benki ya Dunia.
Anatarajiwa kuanza kampeni kali baada ya mkataba wake kutamatika mnamo Agosti mwaka huu.
Hata hivyo, anatarajiwa kurejea nchini mwishoni mwa mwezi huu kuendelea na mikutano yake ya kisiasa huku akitarajiwa kuzindua azma yake ya urais mnamo Agosti.
“Amepeana notisi na anahudumu miezi ya mwisho ya muhula wake. Atakuwa akirejea nchini kuanza kuweka mikakati ya kampeni kabambe baadaye mwezi huu,” akasema Mbunge wa Kitutu Chache Kusini Anthony Kibagendi ambaye ni mwanachama wa sekretariati ya Dkt Matiang’i.
Alisema kurejea kwa Dkt Matiangí kutahusisha mikutano na vigogo wa upinzani anapolenga kujiweka kama mwaniaji anayewaunganisha Wakenya na mwaniaji bora wa kumngóa Rais Ruto 2027.
Ingawa kumekuwa na uvumi na hatihati kuhusu uwanizi wake kwa miezi kadhaa sasa, kujiuzulu kutoka kazi yake ni ishara wazi zaidi kuwa sasa analenga kuwania urais.
Wapanga mikakati ya kisiasa ambao wanashirikiana na Dkt Matiang’i wanasema kuwa analenga kujenga muungano pana wa kisiasa ambao utajikita kwenye umoja, uwazi na maendeleo.
Dkt Matiangí, aliyekuwa naibu rais Rigathi Gachagua ambaye anaongoza chama cha DCP, Kinara wa Wiper Kalonzo Musyoka, Eugene Wamalwa wa DAP-K na Kiongozi wa PLP Martha Karua wamekuwa kwenye muungano moja ambao unalenga kuhakikisha Rais Ruto anahudumu muhula moja pekee.
“Kila mtu lazima ajenge brandi yake kuvutia uungwaji mkono na kuonyesha thamani yake kabla hatujaamua kuhusu mwaniaji ambaye atapambana na Rais Ruto. Hii ina maana kuwa umoja wetu una umuhimu sana,” akasema Bw Kibagendi.
Mbunge huyo alisema watakuwa wakiandaa kura za maoni kuonyesha nguvu, udhaifu na hatua zilizopigwa na kila mwaniaji.
Hakuna fomula ambayo itatumika kumteua mpeperushaji bendera ila umaarufu na uungwaji mkono wake kitaifa ndio utazingatiwa.
Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta ambayo alimuunga mkono Kiongozi wa ODM Raila Odinga mnamo 2022 inasemekana anapigia debe uwanizi wa Dkt Matiangí huku chama chake cha Jubilee kikitangaza kinamuunga mkono waziri huyo wa zamani.
Mnamo Alhamisi Katibu Mkuu wa Jubilee Jeremiah Kioni alisema hatua ya chama hicho kumuunga mkono Dkt Matiang’i inaoana na maoni ya wengi.
“Kwa sasa tukisema kila chama kitamakinikia kuuza mwaniaji wake na kujivumisha kisha baadaye tuunde muungano. Tutao mwaniaji bora ambaye kulingana nasi ni Dkt Matiang’i,” akasema Bw Kioni kwenye mahojiano na Taifa Leo.
Naibu Gavana wa Machakos Francis Mwangangi, mwandani wa Bw Musyoka, alisisitiza kuhusu umoja lakini akasema kila mwanachama wa upinzani yupo huru kumuunga mkono mgombeaji wake.