Habari za Kitaifa

Michuzi ya Uhuru sasa yafuatwa Cherargei akiwasilisha mswada Seneti

Na CECIL ODONGO May 5th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

MVUTANO mpya umeibuka kutokana na juhudi za kumpokonya Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta marupurupu yake ya kustaafu, baada ya hoja kuwasilishwa katika Bunge la Seneti.

Hoja hiyo iliyowasilishwa na Seneta wa Nandi, Samson Cherarkey, anayefahamika maarufu zaidi kama Cherargei, imefungua uwanja mpya wa ubabe wa kisiasa kati ya Bw Kenyatta na Rais William Ruto.

Ubabe huo umechipuka tena kutokana na matamshi ya rais huyo mstaafu wikendi alipohutubia wanachama wa Jubilee katika Kaunti ya Narok wakati wa hafla ya kumkaribisha Katibu Mkuu Moitalel ole Kenta nyumbani.

Kwenye hotuba yake, Bw Kenyatta alikashifu utawala wa Rais Ruto kama unaolenga vyama kama Jubilee inayounga mkono aliyekuwa Waziri wa Usalama wa Ndani Dkt Fred Matiang’i kuwania urais.

Bw Kenytta na Rais Ruto wamekuwa kwenye mvutano mkali wa kisiasa kwa miaka miwili sasa.

Awali zaidi ya Sh1 bilioni zilizotengewa afisi ya Bw Kenyatta zilizuiwa na serikali, kabla ya kurejeshwa kwa marupurupu yake.

Pia, Bw Kenyatta hatimaye aliruhusiwa kufanya kazi katika makazi yake ya Caledonia karibu na Ikulu badala ya afisi iliyokuwa ikitumiwa na mtangulizi wake Mwai Kibaki.

Hoja ya Seneta Bw Cherarkey inataka kuondolewa au kupunguzwa kwa marupurupu ya rais huyo mstaafu japo hatua hiyo imezua mjadala mkubwa bungeni kuhusu mipaka ya kisheria inayosimamia marais wastaafu.

Kwa mujibu wa Sheria ya Malipo ya Pensheni kwa Rais aliyestaafu iliyoanza kutumika mnamo 2003 na kufanyiwa marekebisho 2013, rais aliyekamilisha muhula anastahili malipo ya jumla sawa na mshahara wa mwaka mmoja kwa kila muhula aliotumikia.

Pia anaongezwa pensheni ya kila mwezi inayofikia asilimia 80 ya mshahara wa rais aliye uongozini.

Pia anastahili marupurupu ya burudani ya asilimia 15 ya mshahara wa rais wa sasa, marupurupu ya makazi ya asilimia 23, afisi yenye samani ya hadhi, pamoja na wafanyakazi 34 wakiwemo wasaidizi wa kibinafsi, makatibu, madereva na walinzi.

Bajeti ya mwaka wa fedha wa 2025/2026 imetenga Sh362 milioni kwa marupurupu ya Bw Kenyatta, ikiwa imepungua kutoka Sh448.7 milioni mwaka uliopita.

Aidha, anastahili magari manne (yakiwemo mawili aina ya limousines na mawili ya SUV), marupurupu ya nyumba ya Sh300,000 kila mwezi, mafuta ya Sh200,000, burudani ya Sh200,000, pamoja na bima kamili ya matibabu ndani na nje ya nchi.

Pia lazima awe na pasipoti za kidiplomasia na safari nne za kulipiwa kila mwaka.

Katika hoja yake, Seneta Cherarkey anadai kuwa Bw Kenyatta sasa amerejea kwenye siasa na hali hiyo inaenda kinyume na sheria kwa rais aliyestaafu.

Seneta huyo ameyataja matukio ambapo rais huyo mstaafu amehudhuria na kuhutubia mikutano ya kisiasa, kutoa kauli zinazochukuliwa kuwa za kuunga mkono au kupinga wanasiasa fulani, na kuendelea kujihusisha na kampeni za uchaguzi mkuu wa 2027.

“Vitendo hivyo vinaweza kufasiriwa kama kushiriki moja kwa moja katika siasa za vyama, kinyume na matakwa ya sheria,” akasema.

Hoja hiyo pia inaitaka Bunge kutumia mamlaka yake kupunguza au kuondoa marupurupu hayo, pamoja na kuiagiza Afisi ya Mwanasheria Mkuu kufanya ukaguzi wa kina wa matumizi ya fedha za umma zilizotengwa kwa afisi ya rais huyo mstaafu ndani ya siku 60.

Aidha, inapendekeza kurejeshwa kwa fedha zozote zitakazobainika zilitumika vibaya ili zielekezwe kwenye miradi ya kuwafaa raia.

Jana, Dkt Matiang’i ambaye pia ni naibu kiongozi wa Jubilee alipuuza hoja ya Seneta Cherarkey na kusema ina malengo ya kumdhulumu Uhuru kisiasa.

“Rais Kenyatta amestaafu, ni mwanachama wa Jubilee na anaendelea kutekeleza wajibu wake kama mwanachama. Mwacheni afanye hivyo na serikali imakinikie jukumu la kuwahudumia wananchi.” Aliongeza kuwa rais huyo hayajawa akipokea marupurupu yote tangu astaafu 2022.

Katibu Mkuu wa Jubilee, Bw ole Kenta, naye alisema matamshi ya Bw Kenyatta yalifasiriwa vibaya wala hayakuwa ya kupiga utawala wa sasa vita.

Mvutano kati ya afisi ya Bw Kenyatta na ikulu ulichipuka miaka miwili iliyopita ambapo rais huyo mstaafu alilalamika kuwa afisi yake haifadhiliwi na wafanyakazi wake hawalipwi mishahara.

Hayakukomea hapo pale kulikozuka uhasama mwingine, serikali ikipendekeza Bw Kenyatta atumie afisi ya serikali iliyo Gigiri iliyotumiwa na marehemu Kibaki, lakini Bw Kenyatta akasisitiza atatumia makazi yake ya Caledonia.

Hatimaye, pande hizo zilifikia muafaka ulioruhusu matumizi ya makazi hayo kama afisi rasmi, na kurejesha marupurupu yote kwa mujibu wa sheria.

Sheria ya Bw Cherarkey pia inaweka mipaka kwa marais wastaafu, ikiwataka kutojihusisha moja kwa moja na siasa za vyama, na badala yake kuchukua jukumu la ushauri katika masuala ya kitaifa.

Aidha, Katiba inalinda marupurupu hayo, ikisema hayawezi kupunguzwa kwa hasara ya rais mstaafu wakati wa uhai wake.