Habari za Kitaifa

Nacada yatetea pendekezo la kuongeza umri wa kunywa pombe nchini

Na  NICHOLAS NJOROGE July 17th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

Mamlaka ya Kitaifa ya Kupambana na Matumizi ya Pombe na Dawa za Kulevya (NACADA) imetetea pendekezo lake la kutaka umri wa kisheria wa kunywa pombe nchini Kenya uongezwe kutoka miaka 18 hadi 21, ikitaja utafiti wa kiafya, maoni ya umma na viwango vya kimataifa kama msingi wa pendekezo hilo.

Akizungumza katika kipindi cha Fixing the Nation katika runinga ya NTV jana asubuhi, Naibu Mkurugenzi wa Mipango wa NACADA, Bw Kirwa Lelei, alisema hatua hiyo inalingana na mapendekezo ya Shirika la Afya Duniani (WHO) ambayo yanalenga kulinda afya na maendeleo ya vijana.

Bw Lelei alifafanua kuwa NACADA iliandaa mikutano ya kushirikisha umma katika maeneo 10 ya nchi, ambapo maeneo manane yaliunga mkono kupandishwa kwa umri wa chini wa kunywa pombe hadi miaka 21. Maeneo ya Mombasa na Kaskazini yalisema umri huo upandishwe hadi miaka 25.

Wataalamu wa afya na wanasaikolojia wanaunga mkono pendekezo hilo wakisema ubongo wa binadamu huwa unaendelea kukua hadi kufikia takriban miaka 25. Kuanza pombe mapema kunawaweka vijana katika hatari ya kutekwa na uraibu, hasa kwa walio chini ya miaka 18 ambao wanalewa kutokana na ushawishi wa marafiki na upatikanaji rahisi wa pombe.

“Vijana wengi huanza kunywa pombe kwa kushawishiwa na marafiki na kwa sababu pombe inapatikana kwa urahisi katika mitaa yao,” alisema Bw Lelei.

Takwimu za hivi punde kutoka kwa utafiti wa NACADA zinaonyesha hali ya kutia wasiwasi, ambapo asilimia 2.6 ya wanafunzi wa shule za msingi wamewahi kunywa pombe, asilimia 3.8 kati ya wanafunzi wa sekondari, asilimia 18 wa vyuo vikuu, huku asilimia 23.8 ikirekodiwa miongoni mwa watumishi wa umma. Lelei alisema wanafunzi wa vyuo vikuu ndio wanaoathirika zaidi na unywaji wa pombe.

“Hizi takwimu ni za kushtua na zinaonyesha kwa nini ni muhimu kuzuia mapema,” alisema Bw Lelei.

Bw Lelei alisisitiza kuwa kupandisha umri wa kunywa pombe hadi miaka 21 ni hatua iliyofanikishwa na nchi nyingi duniani, akitaja mfano wa  Amerika ambako hatua hiyo ilipunguza matumizi ya pombe kwa asilimia 16, na Japan ambako kulazwa hospitalini kwa sababu ya matatizo yanayotokana na pombe kulishuka kwa asilimia 20.

Katika kuimarisha utekelezaji hasa katika vyuo vikuu ambako kuna matumizi ya juu ya pombe, NACADA inapanga kushirikiana na wakuu wa vyuo, wachungaji na viongozi wa kidini ili kupambana na ongezeko la uraibu miongoni mwa wanafunzi.