Pasta Gilbert Deya afariki katika ajali ya barabarani
Mhubiri maarufu na mwenye utata, Gilbert Deya, alifariki Jumanne jioni katika ajali ya barabarani iliyotokea katika eneo la Namba Kapiyo, kwenye barabara ya Kisumu kwenda Bondo.
Ajali hiyo iliyohusisha magari matatu: Basi la Chuo Kikuu cha Moi na Toyota Fortuner la Serikali ya Kaunti ya Siaya yaliyokuwa yakitoka Bondo kuelekea Kisian, huku Toyota Noah likitokea upande wa pili.
Mkuu wa Trafiki eneo la Nyanza Bw Peter Maina, alisema kuwa dereva wa Noah alipoteza mwelekeo na kugonga basi.
“Basi hilo lilipojaribu kukwepa kugongana na magari mengine, lilitoka barabarani na kupinduka,” alisema Bw Maina.
Wanafunzi 15 wa Chuo Kikuu cha Moi, waliokuwa wakitoka ziara ya elimu Bondo, walijeruhiwa vibaya na kupelekwa katika Hospitali ya Rufaa na Mafunzo ya Jaramogi Oginga Odinga, Kisumu. Wengine 13 walipata majeraha madogo na kupelekwa katika Hospitali ya Kombewa, Kaunti Ndogo ya Seme.
Wakati huohuo, Noah iligongana na Fortuner, na kusababisha kifo cha dereva wa Noah, ambaye baadaye alitambuliwa kuwa ni mhubiri maarufu Gilbert Deya.

“Tumethibitisha kuwa dereva wa Noah aliyefariki ni Mchungaji Gilbert Deya. Hii ilithibitishwa na mke wake ambaye pia alikuwa ndani ya gari hilo, pamoja na abiria mwingine wa mwanamke,” alisema Bw Maina.
Abiria hao wawili walinusurika wakiwa na majeraha madogo.
Bw Maina aliongeza kuwa uchunguzi wa awali umeonyesha kuwa abiria waliokuwa ndani ya gari la Serikali ya Kaunti ya Siaya hawakuumia.
Mwili wa Mchungaji Deya ulipelekwa katika mochari ya hospitali ya Kombewa.
Kifo cha Ndeya kimewashtua Wakenya wengi, ambao wametuma salamu za rambirambi huku wengine wakikumbuka safari yake tata ya kiroho na mizozo yake ya kisheria.
Mhubiri huyu alipata umaarufu kupitia madai ya kuwa na uwezo wa kuwasaidia wanawake wasio na uwezo wa kuzaa kupata watoto kupitia “nguvu ya maombi”.
Hata hivyo, kufikia mwanzoni mwa miaka ya 2000, serikali za Uingereza na Kenya zilianza kumchunguza, na ripoti kadhaa zilifichua madai ya kutisha ya ulanguzi wa watoto uliokuwa umefichwa kama miujiza ya kiroho.
Mkewe Deya, Mary (anajulikana pia kama Eddah), alikamatwa Nairobi na kuhukumiwa kwa kosa la kuiba mtoto hospitalini.