Ruto At 1,000: Kiu ya mikopo ilikataa kuisha ikimeza Sh1.4 trilioni zingine
LICHA ya ahadi kwamba utawala wake ungebana matumizi na kuhepa madeni, serikali ya Rais William Ruto kufikia Desemba 31, 2024 ilikuwa imekopa jumla ya Sh1.4 trilioni.
Rais Ruto aliyeapishwa na kutwaa mamlaka mnamo Septemba 13, 2022, amekuwa mamlakani kwa muda wa miezi 31, ambayo ni takribani siku 1,000, huku akisalia na miezi 29 kabla ya muhula wake wa kwanza kutamatika hapo Agosti 2027.
Mwenendo huu wa kukopakopa umeiweka Kenya pabaya huku mashirika ya kimataifa ya kutathmini mikopo kama vile Moody, Fitch na S&P yakiibua wasiwasi kuhusu uwezo wa Kenya kudhibiti na kuyalipa madeni yake siku zijazo.
Takwimu za Benki Kuu ya Kenya (CBK), zinaonyesha kuwa kufikia Desemba 31, 2022, miezi mitatu baada ya Rais Ruto kuchukua mamlaka, jumla ya deni la Kenya lilikuwa Sh8.6 trilioni.
Deni hilo ambalo lilikuwa asilimia 67.8 ya Jumla ya Pato la Nchi (GDP) lilijumuisha Sh4.288 trilioni ambazo zilikuwa mikopo ya ndani ya nchi kisha Sh4.29 trilioni zilizokopwa kutoka mataifa ya nje.
Kufikia Desemba 31, 2024, stakabadhi inayochapishwa na Wizara ya Fedha kila mwaka na kuwasilishwa kwa bunge, ilionyesha kuwa deni la nchi lilikuwa limefikia Sh10.6 trilioni.
Hii ilikuwa asilimia 63 ya GDP japo kiwango kisichostahili kupitwa ni asilimia 55 ya GDP.
Kati ya deni hilo la Sh10.6 trilioni, Sh5.2 trilioni ni madeni yaliyokopwa nchini humu huku Sh5.4 trilioni zikiwa madeni kutoka ughaibuni.
Ukirejelea deni la Kenya Kwanza la Sh1.4 trilioni, kufikia Desemba 31, 2024, Rais Ruto alikuwa amekopa Sh741.1 bilioni kwa mwaka.
Pia hii inaweza kufasiriwa kama kukopa Sh2.5 bilioni kila siku, Sh102.9 milioni kila saa na Sh1.7 milioni kwa kila sekunde.
Kinaya ni kuwa wakati ambapo alikuwa akiendesha kampeni, Rais Ruto alitoa ahadi kuwa angeegemea sana kwa uwekezaji badala ya kuendelea kukopa. Nia yake kuu ilikuwa kupunguza deni la taifa ambalo alikiri lilikuwa linailemea Kenya.
“Tutabadilisha mtindo huu wa kuomba mikopo na badala yake tutilie maanani uwekezaji na kufanya miradi ambayo itahakikisha tunabuni nafasi za ajira,” akasema Rais Ruto, wakati huo akiwa naibu rais mnamo Juni 3, 2022 kwenye mkutano wa kisiasa Kamulu, Nairobi.
Rais alitoa ahadi hiyo akifahamu kwamba iwapo angeshinda urais, angerithi uchumi ambao ulikuwa ukiandamwa na madeni mengi makubwa.
Pia alijua kuwa Kenya ilikuwa imetuama katika madeni kutokana na kukopa hela nyingi za China, na pia sakata tele za ufisadi ambazo ziliandama serikali ya Jubilee chini ya Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta.
“Kukopa pesa kuendesha serikali hakutakuwa moja ya mbinu zangu,” akasema Rais akihudhuria mikutano iliyowashirikisha wataalamu wa kiuchumi na fedha.
Katika kampeni, Rais alimsuta mwaniaji wa urais wa Azimio la Umoja-One Kenya Raila Odinga akisema alikuwa anapanga kuendeleza wimbi la kukopa.
“Sisi mbinu yetu ni kutumia njia zilizopo kupata pesa za kuendesha nchi,” akasema akisikitika kuwa asilimia 60 ya mapato ya nchi huelekezwa katika kulipa madeni.
“Kwa sasa kati ya Sh10 tunazokusanya, Sh6 huelekezwa katika kulipa madeni,” akasema Rais wakati wa ibada ya kanisa eneo la Laare, Meru mnamo Septemba 11, siku mbili tu baada ya kuadhimisha mwaka mmoja wa utawala wake.
Mwaka huu wa kifedha, 2025/26, deni la nchi linatarajiwa kuongezeka, serikali ikiunda bajeti ya Sh4.2 trilioni.
Bajeti hiyo ina upungufu wa Sh876.1 bilioni ambapo Sh284.2 bilioni zinatarajiwa kukopwa kutoka nchi, ambazo ni asilimia 1.5 ya GDP.
Sh591.9 bilioni ambazo zitakopwa ndani ya nchi nazo ni asilimia 3.1 ya GDP.
Mikopo hiyo itatolewa kwenye mashirika ya kibiashara kwa sababu Shirika la Kimataifa la Kifedha (IMF) limezima mikopo kwa Kenya hadi Juni 2029.
Mkaguzi wa Bajeti Nancy Gathungu tayari ameonya kuwa bahjeti ya Sh4.2 trilioni kwa mwaka wa kifedha 2025/26 itasababisha serikali ikope fedha zaidi.
Bi Gathungu, alitoa onyo hilo huku Hazina Kuu ya Fedha kupitia Katibu Mkuu, Dkt Chris Kiptoo ikifichua kuwa kufikia Machi 2025, serikali ilikuwa imezidisha pesa zinazokopwa humu nchini kwa mwaka wa kifedha 2024/25 kwa Sh220 bilioni kinyume na kiwango kilichowekwa na Bunge la Kitaifa.
Licha ya kusema asingekopa, mnamo Oktoba 2023, Rais alielekea China akisaka mikopo zaidi.
Shillingi ya Kenya nayo pia inaendelea kuwa dhaifu dhidi ya sarafu za kigeni hali inayoongeza gharama ya kulipa madeni kwa kutumia Dola, Euro na Yuan.
Kwa hivyo kipi kimebadilika? Waziri wa Fedha John Mbadi hakujibu maswali yetu kuhusu hali hii kwenye ujumbe uliotumwa simu inayofahamika.
Hata hivyo, Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti Bungeni, Samuel Atandi alisema uchumi kwa sasa uko katika mkondo mzuri.
“Huwezi kuepuka deni ila lazima sasa tukope kwa hekima tukiendelea mbele,” akasema Bw Atandi. Mbunge huyo wa Alego Usonga alilaumu utawala wa Bw Uhuru Kenyatta kwa kusimamia uchumi vibaya kwa kukopa pesa kisha kufeli kuelekeza hela hizo kwenye miradi ya maendeleo.
Faida kwenye fedha zinazokopeshwa nayo imepanda kutoka Sh171 bilioni wakati wa marehemu rais wa tatu Mwai Kibaki kuondoka mamlakani hadi Sh840 bilioni mnamo 2022.
“Kinachoshangaza ni kwamba katika kipindi hicho, pesa ambazo zimetumika katika miradi ya maendeleo zilikwama katika Sh530 bilioni,” akasema Bw Atandi.
Katika mwaka huu wa kifedha, Kenya inatumia Sh1.2 trilioni kulipa deni la taifa.
Serikali ililenga kukopa Sh263.2 bilioni humu nchini ila kiwango hicho kiliongezwa kwa Sh141.4 bilioni baada ya kutupwa kwa Mswada wa Fedha wa 2024.
Mamlaka ya Ukusanyaji Ushuru (KRA) ilikuwa imepanga kukusanya Sh344.3 bilioni kufadhili sehemu ya bajeti ya Sh3.992 trilioni ambayo iliidhinishwa na Bunge la Kitaifa katika mwaka wa kifedha 2024/25.
Serikali pia imekuwa ikitatizwa na ukusanyaji mdogo wa mapato kuliko shabaha yake. Katika mwaka wa 2023/24 serikali ililenga kukusanya Sh2.5 trilioni lakini ikakusanya Sh2.3 trilioni pekee.
Mwanya uliobakia wa Sh170.4 bilioni ulikuwa upungufu wa asilimia 6.9.
Mnamo 2022/23, mapato yaliyolengwa yalikuwa Sh2.2 trilioni lakini Sh2.1 trilioni ndizo zilikusanywa huku kukiwa na upungufu wa Sh99.35 bilioni.
Ni mnamo 2021/22 ndipo mapato ya serikali yalipita kiwango kilicholengwa kwa Sh101.5 bilioni.
Mwaka huo serikali ililenga Sh1.89 trilioni lakini ikakusanya Sh1.94 trilioni hili likiwa ongezeko la asilimia 5.5.