Habari za Kitaifa

Ruto halali akitupangia lakini hatupati ng’o, wasema viongozi wa Upinzani

Na MOSES NYAMORI, KEVIN CHERUIYOT July 31st, 2026 Kusoma ni dakika: 3

VIONGOZI wa upinzani wameanza mikakati ya kuunda muungano mkubwa wa kisiasa unaofanana na ule wa National Rainbow Coalition (NARC) uliomwingiza madarakani Rais mstaafu Mwai Kibaki mwaka wa 2002.

Mipango hiyo ilibainika jana baada ya kiongozi wa Wiper Patriotic Front (WPF), Kalonzo Musyoka kufanya kikao cha faragha na viongozi wa mrengo wa Linda Mwananchi, ukiongozwa na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna.

Katika muungano wa Narc, vyama vya upinzani na waliokuwa wamehama Kanu waliungana na kumuidhinisha Kibaki kuwania urais kupitia kauli – mbiu maarufu ya Kibaki Tosha iliyobuniwa na aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga.

Kwa mujibu wa duru zilizohudhuria mkutano huo, Bw Sifuna alisema mrengo wa Linda Mwananchi uko katika hatua za mwisho za kusajili chama kipya cha kisiasa.

Viongozi hao walikubaliana kuwa kila upande uendelee kuimarisha ngome zake kisiasa kabla ya kukubaliana kuhusu mgombeaji mwenye uwezo mkubwa zaidi wa kumkabili Rais William Ruto katika uchaguzi mkuu wa Agosti 10, 2027.

Aidha, imebainika kuwa Rais mstaafu Uhuru Kenyatta ameita kikao cha Baraza la Muungano wa Azimio la Umoja-One Kenya kitakachofanyika Jumatatu kujadili mikakati ya uchaguzi huo.

Kiongozi wa Kanu Gideon Moi pia anatarajiwa kuhudhuria kikao hicho, huku aliyekuwa mgombea ugavana wa Nairobi kupitia Kanu, Tony Gachoka, akiwakilisha chama hicho katika mkutano wa Alhamisi.

Kiongozi mmoja wa Linda Mwananchi alisema muungano huo unalenga kuwaleta pamoja viongozi wote wanaotaka Rais Ruto ahudumu muhula mmoja pekee.

“Tutashirikisha makundi yote yanayounga mkono ajenda ya muhula mmoja. Hatimaye kutakuwa na mkutano mkubwa wa vyama vyote vya upinzani na tutaunda muungano mmoja mkubwa kama Narc ya mwaka 2002,” alisema.

Mkutano huo umefanyika wiki moja baada ya viongozi wa Linda Mwananchi kufanya mazungumzo kama hayo na aliyekuwa Waziri wa Usalama wa Ndani, Dkt Fred Matiang’i.

Mbunge wa Suba Kusini Caroli Omondi alisema kundi hilo pia linapanga kukutana na kiongozi wa chama cha DCP, Rigathi Gachagua pamoja na Martha Karua wa People’s Liberation Party (PLP).

Baada ya mkutano huo, Bw Kalonzo alikanusha madai kwamba anafanya mazungumzo ya siri na Rais Ruto kuhusu kujiunga na serikali. Alisema uvumi huo unalenga kudhoofisha umoja wa upinzani lakini hautafanikiwa.

“Ninataka kumwambia William Ruto aache kudhani kwamba Stephen Kalonzo Musyoka anaweza kujiunga naye. Tutakutana naye kwenye sanduku la kura mwaka wa 2027,” alisema.

“Nasi viongozi wa upinzani, Sifuna, Gachagua au mimi, yeyote atakayekubali kuungana na Ruto, atapata adhabu kali kutoka kwa raia.”

Kalonzo alisisitiza kuwa ataendelea kushirikiana na vyama vingine vinavyotaka kuondoa Kenya Kwanza mamlakani kupitia uchaguzi.

Kwa upande wake, Seneta Sifuna alisema Wakenya wanataka kuona upinzani ulioungana na wenye uwezo wa kutoa uongozi mbadala.

“Tutazungumza na viongozi wote wa upinzani ili kujenga mwafaka. Hatutaki kuwaangusha Wakenya ambao wanatarajia kuona viongozi wakifanya kazi pamoja,” alisema.

Awali, Sifuna aliwahi kusema Linda Mwananchi iko tayari kushirikiana na yeyote anayepinga muhula wa pili wa Rais Ruto, akiwemo Bw Gachagua.

Hata hivyo, licha ya kauli za umoja, kuna hofu kuwa maslahi ya kisiasa yanaweza kuvuruga mipango hiyo.

Kalonzo, Gachagua, Sifuna, Dkt Matiang’i, Martha Karua na kiongozi wa DAP-K Eugene Wamalwa wote wameonyesha nia ya kuwania urais.

Wachambuzi wa siasa wanasema changamoto kubwa haitakuwa kuunda muungano bali kukubaliana kuhusu mgombea wa urais na mgombea mwenza, huku masuala ya ushawishi wa kikanda na usawa wa kisiasa yakitarajiwa kuwa muhimu.

Historia inaonyesha migawanyiko imeigharimu upinzani mara kadhaa.

Mwaka 1992, vyama vya upinzani vilishindwa kuafikiana kuhusu mgombea mmoja na hivyo kumpa aliyekuwa Rais Daniel arap Moi ushindi mwingine.

Hali kama hiyo ilijirudia mwaka wa 1997 na tena mwaka wa 2007, ambapo mgawanyiko kati ya Raila Odinga na Kalonzo Musyoka uliwanufaisha wapinzani wao na kuchangia mvutano mkubwa baada ya uchaguzi.

Kutokana na historia hiyo, viongozi wa sasa wa upinzani wanajaribu kuepuka makosa yaliyopita kwa kuanza mazungumzo mapema ili kuunda muungano mmoja wenye uwezo wa kumpa Rais Ruto ushindani mkali katika uchaguzi wa 2027.

Jana, Bw Musyoka alisema kinara yeyote wa upinzani atakayezungumza na Rais Ruto atatengwa na wenzake akisema hakuna aliye tayari kusaliti Wakenya.

“Hatutasaliti hisia za taifa, atakayesikika alikutana na Ruto, awe ni Sifuna au rafiki yangu Rigathi Gachagua, huo utakuwa mwisho wa kushirikiana nasi,” alisema msimamo ambao Sifuna alikubaliana nao.