Habari za Kitaifa

Ukatili wa kutisha mama, binti na mpwa walioishi Eastleigh wakiuawa na miili kutupwa maeneo tofauti

Na HILLARY KIMUYU October 24th, 2024 Kusoma ni dakika: 2

WAKAZI wa mtaa wa Eastleigh wamebaki kwa mshangao baada ya mwanamke, bintiye na mpwa wake kuuawa kikatili na miili yao iliyokatwakatwa kutupwa katika maeneo tofauti Nairobi na Machakos.

Mwanamke huyo, aliyetambulika kama Waris Daud, bintiye Amina Abdirashid mwenye umri wa miaka 21, na mpwa wake Nuseiba Dahir mwenye umri wa miaka 12 walitoweka Jumatatu usiku, kulingana na polisi.

Siku ya Jumanne, familia yao ilipokea habari za kuhuzunisha kwamba mwili wa jamaa zao ulikuwa umegunduliwa Parklands, na mwingine huko Bahati, huku mabaki ya mama yao yakipatikana msituni huko Machakos-wote waliuawa kwa njia sawa.

Mwili wa Amina, ambao ulikuwa nusu uchi ukiwa na majeraha yanayoonekana, ulipatikana kwenye Barabara ya Mwambo saa kumi na mbili asubuhi Jumanne.

“Mwili ulikuwa na majeraha kadhaa ya kudungwa kisu mgongoni, kifuani, mikononi na kichwani. Eneo hilo lilionekana kutovurugwa na hakukuwa na dalili za mapambano,” inasema sehemu ya ripoti ya polisi iliyoonekana na Taifa Leo.

Saa mbili baadaye, mwili wa Nuseiba ulipatikana umetupwa kando ya Shule ya Msingi ya Bahati katika Kaunti ndogo ya Kamukunji, ukiwa na nguo zilizotapakaa damu lakini haukuwa na majeraha yoyote.

‘Karibu na mwili huo kulikuwa na kiatu na nguo ya ndani inayoaminika kuvaliwa na marehemu,’ polisi walisema.

Maafisa wa polisi pia walipata kisu kwenye eneo la tukio.

‘Kulikuwa na alama za tairi za gari linaloshukiwa kuwa katika eneo la uhalifu. Polisi wanaamini kuwa gari hilo ambalo halijatambuliwa lilitumiwa kuusafirisha mwili huo.”

Kamanda wa Polisi wa Kaunti Ndogo ya Athi River Kusini, Philis Muthoni Jumatano alithibitisha kuwa mwili wa mwanamke ulipatikana karibu na Shule ya Sekondari ya Alim kwenye barabara ya Kyumbi-Machakos, eneo la Kyamutheke Tarafa ya Kinanie.

‘Watu waliripoti mwili wa wa mwanamke kike uliokuwa umetupwa karibu na shule na maafisa wa polisi Machakos, waliuchukua,’ alisema.

Kwa mujibu wa kamanda huyo, mwili huo ulikuwa umekatwakatwa na ilionekana kuwa wauaji walitumia kitu chenye ncha kali kumuua.

Mikono ya Waris ilikuwa imekatwa na haikupatikana eneo la tukio.

“Pia alikuwa na majeraha makubwa usoni, masikio yake yalikuwa yamekatwa, macho yake yalikuwa yameng’olewa na shingo yake. Alikuwa amenajisiwa,” aliongeza.

Polisi wanashuku kuwa, sawa binti na mpwa wake, mwanamke huyo aliuawa kwingine na mwili wake kutupwa karibu na shule.

Miili hiyo miwili iliyopatikana Nairobi ilipelekwa mochari ya Nairobi, huku wa mama yao ukihifadhiwa katika mochari Machakos.

Picha za CCTV karibu na ghorofa walimokaa waathiriwa hao watatu, zilizoonekana na Taifa Leo, zinaonyesha wasichana hao wawili wakipanda teksi mwendo wa saa tisa usiku wa kuamkia Jumatatu na hiyo ilikuwa mara ya mwisho kuonekana wakiwa hai.

Kamanda wa polisi wa Nairobi Adamson Bungei alithibitisha kuwa kitengo cha kuchunguza mauaji kimechukua jukumu la uchunguzi.

‘Bado hatujui ni kwa nini hii ilitokea, lakini timu zetu zinaendelea na uchunguzi ili kujua kilichofanyika,’ Bungei alisema.

Imetafsiriwa na BENSON MATHEKA