Ziara ya Ruto Nyanza mtihani mkubwa baada ya kifo cha Raila
ZIARA ya siku tano ya Rais William Ruto katika eneo la Nyanza kuanzia Jumapili, Septemba 13, imeibua mjadala mpana wa kisiasa huku wachambuzi wakisema ni zaidi ya ziara ya kawaida ya kukagua na kuzindua miradi ya maendeleo.
Ziara hiyo inafanyika katika kipindi nyeti kisiasa baada ya kifo cha aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga, jambo lililoacha pengo kubwa la uongozi katika eneo ambalo kwa miongo kadhaa lilikuwa ngome yake ya kisiasa.
Rais Ruto anatarajiwa kuzuru kaunti za Kisumu, Siaya, Migori na Homa Bay akizindua na kukagua miradi mbalimbali ikiwemo barabara, maji na usafi wa mazingira, masoko, hospitali, nyumba za gharama nafuu, viwanja vya michezo pamoja na miundombinu mingine ya umma.
Mbali na kuhudhuria ibada ya kanisa Kisumu, Rais pia anatarajiwa kukutana na viongozi mbalimbali na hata kuendesha kikao cha Baraza la Mawaziri katika Ikulu Ndogo ya Kisumu.
Kwa serikali ambayo imekuwa ikitumia maendeleo kama silaha yake kuu ya kisiasa, ziara hiyo ni nafasi muhimu ya kuwashawishi wakazi wa eneo ambalo kwa muda mrefu lilimuunga mkono Raila Odinga na chama cha ODM.
Hata hivyo, umuhimu wa kisiasa wa ziara hiyo unazidi miradi inayozinduliwa. Kifo cha Raila Odinga mnamo Oktoba 15, 2025, kiliondoa mwanasiasa aliyekuwa na ushawishi mkubwa zaidi katika Nyanza na kuacha swali kubwa kuhusu ni nani atakayerithi mtandao wake wa kisiasa na kura zake.
Katika mahojiano maalum yaliyopita, Rais Ruto alikiri kuwa uwepo wa Raila ungeathiri kwa kiasi kikubwa mazingira ya kisiasa ya sasa.
Alimtaja Raila kama mwanasiasa wa kipekee aliyekuwa na ujasiri, maono na uelewa wa masuala ya taifa. Vilevile alisema yeye na Raila walikuwa na sera walizokubaliana, ikiwemo mpango wa nyumba za gharama nafuu na huduma ya afya kwa wote.
Ruto sasa anaonekana kutaka kuwashawishi wakazi wa Nyanza kuwa ushirikiano kati ya serikali yake na viongozi waliokuwa karibu na Raila unaweza kuendelea kunufaisha eneo hilo.
Tayari baadhi ya viongozi wa zamani wa ODM wanahudumu katika serikali yake, akiwemo Waziri wa Kawi Opiyo Wandayi, Waziri wa Fedha John Mbadi, Waziri wa Madini Hassan Joho na Waziri wa Vyama vya Ushirika Wycliffe Oparanya.
Kwa mujibu wa wachambuzi wa siasa, Rais atajaribu kuunganisha ujumbe wa maendeleo na ujumuishaji wa kisiasa kwa kuonyesha kuwa Nyanza haifai kuwa upande wa upinzani ili kupata rasilimali za kitaifa na uwakilishi serikalini.
Lakini upinzani pia unajipanga. Makundi mbalimbali yanayowania urithi wa kisiasa wa Raila tayari yameanza kufanya ziara katika eneo hilo. Miongoni mwao ni vuguvugu la Linda Mwananchi ambalo limekuwa likisisitiza kuwa maendeleo peke yake hayawezi kuchukua nafasi ya uwajibikaji, utawala bora na kuheshimiwa kwa Katiba.
Hali hiyo inakita ujumbe wa serikali wa maendeleo dhidi ya ujumbe wa upinzani unaojikita katika masuala ya utawala.
Katika kaunti ya Kisumu, Rais anatarajiwa kuzindua mnara wa kudhibiti safari za ndege katika uwanja wa ndege, kukagua makao ya polisi na kuzuru barabara ya Mamboleo-Miwani-Chemelil-Muhoroni pamoja na miradi ya maji. Atazuru pia sekta ya Jua Kali.
Katika Siaya, atakagua Daraja la Dhogoye, hospitali ya Siaya, miradi ya makazi, viwanja vya michezo na mtandao wa barabara katika maeneo ya Bondo, Ugenya, Alego Usonga na Rarieda.
Mbunge wa Bondo Gideon Ochanda amesema Daraja la Dhogoye yatakuwa hatua kubwa kwa wakazi kutokana na umuhimu wake katika kurahisisha mawasiliano, usafiri na biashara.
Migori nayo iko katika ratiba ya Rais ambapo atakagua barabara katika maeneo ya Uriri, Awendo na Suna Mashariki pamoja na kituo cha umeme cha Masaba katika Kuria Magharibi.
Katika Homa Bay, Rais anatarajiwa kuzindua masoko, barabara za mji na miradi ya taasisi ya mafunzo ya matibabu ya KMTC ya Sindo.
Wakati huo huo, viongozi wa eneo hilo wanataka miradi mikubwa kama Bwawa la Koru-Soin, Uwanja wa Moi Stadium na barabara ya Mamboleo-Miwani-Chemelil kukamilishwa haraka.
Hatua za usalama pia zimeimarishwa kufuatia tukio la hivi majuzi Siaya ambapo vijana walidaiwa kujaribu kuzuia msafara wa viongozi waliohudhuria hafla ya kuwawezesha wanawake kiuchumi iliyoongozwa na Mama wa Taifa Rachel Ruto.
Kamishna wa eneo la Nyanza, Onesmus Kyatha, amesema ziara hiyo inalenga maendeleo na kwamba maandalizi yote ya usalama yamekamilika ili kuhakikisha shughuli zinaendeshwa kwa utulivu.