Habari

Hatutawalinda polisi wanaotumia vibaya silaha zao, Rais aonya

Na NDUBI MOTURI June 14th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

RAIS William Ruto ameahidi Wakenya kwamba, maafisa wa polisi wanaotumia silaha na mamlaka yao vibaya watawajibikia vitendo vyao.

Akizungumza katika hafla ya kuteketeza zaidi ya bunduki haramu 6,000 katika Chuo cha Kitaifa cha Mafunzo ya Uongozi wa Polisi kilichoko Ngong, Rais alisifu mpango wa kuboresha huduma ya polisi kwa kima cha Sh9 bilioni akisema, serikali imejitolea kuboresha mafunzo na vifaa vya maafisa wa usalama.

“Tumejitolea kuboresha huduma ya polisi kupitia mafunzo na vifaa vya kisasa kwa makamanda wetu ili waweze kutoa uongozi bora kwa walio chini yao. Lazima tulinde maisha ya Wakenya. Ikiwa kuna maafisa wa polisi waliopotoka, watashughulikiwa ipasavyo,” alisema Dkt Ruto.

Hafla hiyo ilihudhuriwa na wawakilishi wa serikali kutoka nchi 15 wanachama wa Kituo cha Kikanda cha Kukabiliana na Silaha Haramu(RECSA).

RECSA ni shirika la serikali za nchi mbalimbali lililo na jukumu la kuratibu utekelezaji wa kuzuia, kudhibiti na kupunguza silaha haramu katika Ukanda wa Maziwa Makuu, Upembe wa Afrika na mataifa jirani.

Mataifa wanachama wa RECSA ni pamoja na Burundi, Jamhuri ya Afrika ya Kati, Jamhuri ya Congo, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Djibouti, Ethiopia, Eritrea, Kenya, Rwanda, Ushelisheli, Somalia, Sudan Kusini, Sudan, Uganda na Tanzania.

Afisa Mkuu Mtendaji wa RECSA, Bw Jean Pierre, alisema serikali zinatazamia kuimarisha ushirikiano na matumizi ya teknolojia ili kuongeza usalama katika ukanda huo.

“Tunapoadhimisha miaka 20 ya juhudi za kuangamiza silaha haramu, tunakubali kuwa ushirikiano na kubadilishana taarifa ni muhimu sana. Tumefanikisha ushirikiano ambao unalenga kukabiliana na changamoto za kikanda,” alisema Bw Pierre.

Silaha zilizoteketezwa zilipatikana kati ya mwaka 2022 na 2025, zilizosalimishwa kwa hiari na raia au kukamatwa katika oparesheni mbalimbali za polisi kote nchini.